November 14, 2012

November 13, 2012

Mambo ya Kufanya Baada Ya Kuokoka:


  • Sijui kama wewe umewahi kusikia au kushuhudia,lakini mimi nimeshawahi kushuhudia watu wengi waliochukua uamuzi wa kuokoka wakiacha maisha mazuri ya wokovu ndani ya Yesu na kurudia maisha yao ya zamani.Wengine walishaanza hata kumtumikia Mungu kwa huduma mbalimbali lakini wakarudi nyuma.Ni dhahiri kabisa kuwa si mapenzi ya Mungu mtu wake aamue kuokoka halafu arudi tena nyuma.Kiu ya Mungu ni kuona watu wake wanokoka na wakishaokoka waendelee kusonga mbele kwenye maisha ya wokovu mpaka siku ya kufa kwao au mpaka siku Bwana Yesu atakaporudi mara ya pili kama bado watakuwa hai.

    Ni vyema basi wewe ambaye umeamua kuokoka kufahamu baadhi ya mambo yatakayokusadia ili udumu katika wokovu maisha yako yote.

    Baadhi ya mambo yawafanyayo watu wa Mungu kurudi nyuma katika maisha ya wokovu:

    Kutokusoma Neno la Mungu(Biblia) kwa bidii.

    Kutokuwa waombaji wa bidii.

    Kutokuwa na ushirika na waliokoka wengine.

    Kutokupata watumishi wa kuwalea kiroho na kuwatia moyo.

    Kuona aibu kukiri wokovu wao mbele ya wanadamu.


    Mambo ya Kufanya Baada Ya Kuokoka:

    1. Soma Neno la Mungu kwa bidii sana kila siku,mara nyingi iwezekanavyo.Mara baada ya kuokoka wewe ni mtoto mchanga kiroho,Biblia inasema utumie maziwa yasiyoghushiwa(Non-diluted milk)ya kiroho ambayo ni Neno La Mungu(1Petro2:2).Neno la Mungu litakujengea ndani yako nguvu za Mungu za kukuwezesha kudumu katika wokovu siku zote.Ni muhimu basi ujiwekee ratiba yako ya kusoma Biblia yako kila siku na kuhudhuria mikutano na semina za Neno la Mungu wetu.

    2. Kuwa muombaji kwa bidii,Baada ya kuokoka sasa unatakiwa uwe mwombaji sana.Biblia inasema wazi kwenye Yakobo 5:16b:"....Kuomba kwake mwenye haki kwafaa sana kama akiomba kwa bidii",Kinachotakiwa sii kuomba tuu,bali kuomba kwa bidii.Ukimwomba Mungu anasikia na atakujibu maombi yako sawasawa na mapenzi yake.

    3. Acha dhambi;ndugu mpendwa,baada ya kuokoka sasa unatakiwa KUACHA kila dhambi uliyokuwa unaifanya kabla ya kuokoka,unatakiwa uanze maisha mapya kabisa ya kumtukuza Mungu.Ukishaokoka Mungu anakusamehe dhambi zako zote nawe sasa usifanye dhambi tena.Muombe Mungu akupe nguvu zake ile usifanye dhambi tena,hii inawezekana kabisa.

    4. Kuwa na Ushirika na watu wengine waliookoka,ni wazi kuwa watu walio karibu sana na mtu wana uwezo mkubwa sana wa kumbadilisha mtu huyo mawazo yake.Hivyo basi baada ya kuokoka nawe ni muhimu sana ukawa na uhusiano wa karibu sana na watu wengine ambao wameshaokoka,hao watakushauri namna ya kudumu na kukua katika wokovu,watakujibu na maswali ambayo unaweza kuwa nayo.Hata kama watu walijua kama wewe hujaokoka,wafahamishe kuwa umeokoka na kuwa unataka uwe karibu nao.

    5. Kuwa karibu na watumishi mbalimbali wa Mungu,uwaeleze juu ya uamuzi wako wa kuokoka,waombe wakuombee maana ni Kazi waliyopewa na Mungu.Usiwaogope watumishi wa Mungu bali jenga nao urafiki wa karibu sana.Hudhuria Fellowships,mikutano ya Injili na Semina za Neno La Mungu mara kwa mara.

    6. Wafahamishe wenzako kuwa sasa Umeokoka,Ni muhimu sana kuwafahamisha na wengine uamuzi wako wa kuokoka.Hii itakusaidia kwani wakishafahamu kuwa umeokoka hawatakushirikisha tena mambo ambayo ni mabaya(yawe maneno,maandishi,picha au hata matendo)hii itakusadia wewe kukua haraka sana kiroho.

    7. Usife moyo,Ndugu,katika maisha ya wokovu hatutakiwi kuvunjika moyo.Mara baada ya kuokoka inawezekana shetani akataka kukutisha tamaa ya kudumu katika wokovu(kumbuka!shetani hajafurahi kuona wewe umeokoka)ili umrudie yeye.Anaweza akakuletea watu wa kukukashifu ili uacha wokovu au kukushauri uache wokovu au akatumia mbinu zozote zile zikiwemo majaribu mbalimbali.Watu wengi wanafikiri wakiokoka basi ndio haukuna tena majaribu(magumu),mpendwa kuokoka sio mwisho wa majaribu bali ni mwanzo wa majaribu lakini na USHINDI JUU.(Warumi 8:28,37)Unapaswa kufahamu kuwa hakuna jaribu limpatalo mwanadamu Mungu asipotoa njia ya kushinda,kwenye kila jaribu kuna msaada wa Mungu wa kukusaidia,Ukikutana na majaribu hayo wewe dumu kwenye maombi na usirudi nyuma kamwe.

    Hayo ni baadhi tuu ya Mambo ambayo ninapenda uwe nayo unaipoianza safari hii ya wokovu.Tafadhali wasiliana na mimi kwa ushauri zaidi.
     
-2007