September 17, 2011

SOMO LA UTAKATIFU



1. Je, Utakatifu Ni Nini?
Jibu lake ni rahisi, neno utakatifu lina maana ya kutengwa kwa ajili ya Mungu Baba, na kumwishia Yeye kwa namna inayompendeza. Utakatifu unaonekana katika maisha ya Yesu, na katika maisha ya mkristo anayekua kiroho. Ni mfumo wa maisha ambao Mungu anautaka kwa watu wake anaowaita watakatifu.
2. Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu, Bwana Mungu Mwenye Uweza
Je ulijua kwamba Mungu si mtakatifu mara moja tu, lakini kwa sababu ya nafsi tatu zinazofanya Mmoja, yeye ni mtakatifu mara tatu? Ndivyo anavyosifiwa mbinguni na duniani (Isa 6:3) (Ufu 4:8).
Yesu alisema,”Baba Mtakatifu” (Yn 17:11).
Yesu ni Mtakatifu na Mwenye Haki (Mdo 3:14).
Roho wa Mungu ni Roho wa utakatifu (Rum 1:4).
3. Mwe Watakatifu, Kwa Kuwa Mimi Ni Mtakatifu
Watoto wafanane na Baba yao; huo ndio mwito wa Mungu kwa kila mmoja katika familia yake. Yafaa watu wamfahamu Baba yetu kwa kututazama sisi (1Pet 1:15, 16). Sisi ~
Tumechaguliwa kuwa watakatifu (Efe 1:4).
Tumeitwa kuwa wanaume na wanawake watakatifu (1The 4:7).
Tumeitwa kuwa kanisa takatifu (1Kor 1:2).
Tumepewa neema ya kuwa watakatifu (2Tim 1:9).
4. Aina Mbili Za Utakatifu
Kwanza kabisa, kuna kazi ambayo Kristo mwenyewe aliikamilisha pale Msalabani ya kutusamehe dhambi zetu na kututakasa; hiyo peke yake inatufanya watakatifu na kukubalika mbele za Mungu. Utakatifu huu hautokani na lo lote tunalofanya au tusilofanya. Sisi tumefanywa watakatifu kwa sababu katika neema yake Yesu alitwaa kutoka kwetu hali ya kukosa utakatifu na badala yake akatupatia utakatifu wake mwenyewe, la sivyo tusingeweza kamwe kuingia kwenye uwepo wa Mungu (Ebr 2:11; 13:12; 10:10).
Ni Mwanzo Tu, Bado Hatujakamilika
Lakini ingawa tumefanywa watakatifu mbele za Mungu, katika uzima na kuishi bado tunaendelea kufanywa watakatifu. Mapambano dhidi ya dhambi, ubinafsi na Shetani, na safari ya kuelekea kwenye ukamilifu wa maisha matakatifu Kutakuwa na kuanguka kwingi na kushindwa kwingi njiani (Ebr 10:14).
5. Tunataka Kuwa Watakatifu, Lakini Kwa Namna Gani?
Je, hili ni suala la mtu kuamua kuwaza mawazo mazuri zaidi, kusema maneno ya upole zaidi na kufanya mambo mema zaidi mara kwa mara? Maamuzi yote ya jinsi hiyo hayafai kitu kama watu wengi wanavyofahamu.
Mapambano Kati Ya Kujihesabia Haki Na Neema
Kutokana na hali ya kutaka kuwa safi na watakatifu, vizazi vya waamini wamefikia hatua ya kujihesabia haki kuhusiana na namna wakristo wanavyopaswa kuishi, wakibeba na kuwatwisha wengine mizigo ya sheria. Sheria zenyewe wakazivunja, na hivyo kushindwa.
Sheria
Mwamini anayejihesabia haki hutafakari kuhusu ni lipi afanye au ni lipi asifanye kwa kujiuliza mwenyewe iwapo mambo kama dansi, mvinyo, fedha, fasheni, sinema, na mitindo ya nywele ni uovu au hayana maana kwa wakristo. Anafanya maamuzi, anajidhibiti mwenyewe na kuwahamasisha wengine kuifuata sheria yake mpya. Matokeo yake wakristo wengi mara kadhaa wameshindwa kuwa chumvi na nuru katika shughuli mbalimbali za hadhara, na hivyo kuwafanya wasioamini bado kujichagulia mwelekeo wao wenyewe.
Neema
Neema inasema kwamba hakuna hata moja katika hayo lililo ovu au ambalo halina maana kwa wakristo; la msingi hapa ni namna tunavyoamua kutumia vitu hivyo. Kwa mfano, neema inasema kwamba uovu uko kwenye matumizi ya pombe na sio pombe yenyewe. Uovu uko katika kupenda fedha na sio fedha zenyewe. Hakuna uovu katika kucheza dansi ila katika sababu za kucheza.
Tusonge mbele Na Roho Mtakatifu
Iwapo utaamua kuchagua sheria au neema kuwa mtindo wa maisha yako, lakini ujue kwamba utakatifu wa kweli unapatikana kwa Roho Mtakatifu pekee ambaye asili yake ni utakatifu kama jina lake mwenyewe lilivyo – Mtakatifu.
Kujazwa kila siku na Roho Mtakatifu maana yake ni kwamba mwili, nafsi, na roho ya mwamini wakati wote anaendelea kuwa amefurika kwa kujawa na huyo mtu mtakatifu; akiendelea kuchuja kila wazo, neno na tendo la huyo mwamini , na kuwa mvumilivu katika kumletea maisha matakatifu kwa ndani, maisha yanayokubaliana na kila neno la Mungu, lakini yasiyotegemea juhudi za kibinadamu. Mara atafanya uwepo wake kujulikana, na unapofanya kosa au kutamka neno ovu, anashuhudia ndani ya moyo wako.
6. Njia Ya Utakatifu
Matakwa yetu na maamuzi yetu ni muhimu katika njia ya utakatifu. Kazi ya Maandiko ni kutuelekeza. Hapa kuna changamoto moja kutoka katika Kum 22:9-11:
Usipande aina mbili za mbegu katika shamba lako la mizabibu; ukipanda, utakuwa umetia unajisi mazao uliyopanda pamoja na matunda yake.
Usilime shamba kwa kuwafunga pamoja ng’ombe na punda kwenye kongwa moja.
Usivae nguo yenye mchanganyiko wa sufu na pamba.
Kataa Mchanganyiko Wa Mbegu Usio Mtakatifu
Mbegu zinapopandwa na kumwagiliwa hutoa mazao yanayofanana nazo. Kwahiyo panda mbegu moja tu ya neno la Mungu, yaani kweli; na kamwe usichanganye kweli ya Mungu na hekima ya ulimwengu huu, la sivyo utavuna zao la kuchanganyikiwa.
Kataa Mchanganyiko Wa Ushirika Usio Mtakatifu
Ni watu wawili pekee wanaompenda Mungu na wanaoamini Maandiko wanaoweza kuwa mmoja katika ndoa, au wamoja katika biashara. Soma yale aliyoyasema Paulo kwa habari ya kufungiwa nira katika 2Kor 6:14-17.
Kataa Mchanganyiko Wa Mavazi Usio Mtakatifu
Uvaaji aliotupa Mungu ni vazi la haki na kufunikwa na uweza utokao juu. Ikiwa leo tutavaa mavazi ya Mungu na kesho tukavaa mavazi ya ulimwengu, kamwe hatutakuwa watakatifu, na wala hatutafanana na jinsi ambavyo Baba anataka sisi tuwe (Isa 61:10) (lk 24:49). Njoo Ee Roho Mtakatifu utujaze na kutusaidia.

0 comments:

Post a Comment