September 17, 2011

Utakaso- Kukamilisha Utakatifu



Utakaso- Kukamilisha Utakatifu
 
“Njooni kwangu ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na             mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi” (Mathayo 11:28-30).

Wanaojiita Wakristo wachache sana wangebisha kwamba mistari hiyo hapo juu ni mwaliko kutoka kinywani kwa Yesu, akiwaita watu waokoke. Mara nyingi sana maandiko hayo hutumiwa kwenye mikutano ya uinjilisti. Yesu alikuwa anatoa pumziko kwa waliochoka. Bila shaka hakuwa anasema juu ya mapumziko kimwili kwa waliochoka kimwili. Alikuwa anaahidi pumziko kwa ajili ya nafsi au roho (ms. 29) ambazo zimelemewa na dhambi na hatia. Alikuwa anatoa wokovu. Lakini, wokovu huo unapokelewaje? Yesu alisema unapatikana kwa kujitia nira Yake.
Labda tafsiri inayopendwa sana na wale wanaopinga kushika sheria kuhusu maana ya kujitia nira ya Yesu ni hii: Fikiri kwamba Yesu amevaa nira yenye pande mbili ambayo anataka tuishiriki. “Uthibitisho” wa tafsiri hiyo ni kwamba Yesu anasema hiyo nira ni “Yangu” kuonyesha kwamba bila shaka ni nira ambayo iko shingoni Mwake. Sasa, yule asiyeamini kushika sheria anasema, “Sawa! Yesu hamaanishi kwamba anataka kuihamishia hiyo nira shingoni mwangu kutoka Kwake. Maana yake ni kwamba amevaa nira yenye sehemu mbili, kwa ajili ya maksai wawili! Basi, anataka mimi “nifungiwe nira” na Yeye kwa imani, ili tuunganishwe pamoja katika safari yetu kwenda mbinguni.”
Lakini, hiyo tafsiri ambayo imekwenda mbali kiasi hicho inakosa kuelewa kitu. Kujitia nira ya Yesu ni mfano wa kujinyenyekeza chini ya mamlaka Yake. Yeye hana nira yenye pande mbili shingoni kwake ambayo anataka sisi tushirikiane Naye kuivaa. Yeye – kama Bwana – ameshikilia nira mikononi Mwake, akiwa amesimama mbele ya maksai wote ambao hawajafugwa, ambao wakati huu wanahangaika na mizigo ya hatia, wakiwa wametiwa nira na dhambi. Anawaita akisema, "Mkitaka pumziko, kuna njia moja tu ya kulipata. Jitieni nira Yangu. Mimi nataka kuwa Bwana wenu, lakini lazima mkubali kujinyenyekeza kwangu. Fanyikeni wanafunzi Wangu, jifunzeni kwangu, na ule mzigo mzito ulioko nafsini mwenu utaondoka. Nira nitakayoweka kwako itakuwa laini, na mzigo nitakaokupa ni mwepesi, kwa sababu Roho Wangu Mtakatifu atakuwezesha kunitii. Ukiisha kuniamini na kukubali kuwa chini ya mamlaka yangu kama Bwana, utazaliwa upya kiroho; ndipo amri Zangu hazitakuwa mzigo kwako” (ona 1Yohana 5:3). Huu ndiyo ujumbe wa Yesu kuhusu wokovu, usiobadilika.
“Kujitia nira” ni mfano wa kuwa chini ya mamlaka ya mwingine. Mara kwa mara Maandiko hutumia huo mfano wa nira kwa njia hiyo. Wale wanaomwamini Yesu kweli hukubali kuwa chini ya mamlaka Yake. Maksai aliye na nira ana sababu moja tu ya kuwepo kwake: kufanya huduma ya bwana wake. Anaweza asijue bwana wake anataka afanye nini hasa, lakini mapenzi yake anayakubali. Yu tayari kwenda kazini.
Utakaso Unafafanuliwa
Hii sura inahusu utakaso, au, kuongezeka kwa utakatifu kunakotokea kwa wale waliozaliwa mara ya pili. Maana ya kutakaswa ni “kutengwa kwa ajili ya kutumiwa kwa kazi takatifu.” Basi, ni neno lenye kueleza mpango wa Mungu kwa ajili ya kila aaminiye vizuri sana. Agano Jipya linatumia neno hilo kwa hali mbili: wakati uliopita na wakati uliopo. Waamini wametakaswa na wanaendelea kutakaswa. Neno la wakati uliopita linadhihirisha nia ya Mungu – ametusamehe dhambi zetu na kutupa Roho Wake Mtakatifu ili kututenga kwa ajili ya matumizi matakatifu. Neno la wakati wa sasa linadhihirisha ile hali inayoendelea ya kutimizwa kwa kusudi Lake – tunaendelea kutumiwa kwa makusudi matakatifu ya Mungu, na kuzidi kufanya hivyo.
Bahati mbaya ni kwamba, kwa wengi wanaojiita Wakristo, utakaso si kitu zaidi ya nadharia kwa sababu hawajawahi kuzaliwa mara ya pili, ambacho ni kitu cha lazima kwa ajili ya utakaso. Lakini wengi wanaamini kwamba wamefanywa kuwa wenye haki ndani ya Kristo ingawa hakuna ushahidi wowote wa utakaso maishani mwao. Lakini, Maandiko yanatuambia kwamba pamoja na kuhesabiwa haki, utakaso huja.
Bali kwa yeye ninyi mmepata kuwa katika Kristo Yesu, aliyefanywa kwetu … haki na utakatifu na ukombozi … Na baadhi yenu mlikuwa watu wa namna hiyo; lakini mlioshwa, lakini mlitakaswa, lakini mlihesabiwa haki katika jina la Bwana Yesu Kristo, na katika Roho wa Mungu wetu (1Wakor. 1:30; 6:11 – Maneno mepesi ni kutilia mkazo).
Yohana naye aliandika hivi:
Kama mkijua ya kuwa yeye ni mwenye haki, jueni ya kuwa kila atendaye haki amezaliwa na yeye … Watoto wadogo, mtu na asiwadanganye; atendaye haki yuna haki, kama yeye alivyo na haki (1Yohana 2:29; 3:7).
Wengi wanaojiita Wakristo watasikiliza kwa furaha mahubiri yenye kuangukia katika fungu liitwalo “mahubiri ya utakaso”, ambayo yanawahimiza “kutoa” maeneo mbalimbali ya maisha yao kwa Kristo ili ayatawale. Lakini, inaishia hapo kwa sababu kweli hawawi na nia ya “kutoa” eneo lolote la maisha yao kwa Kristo, hasa kama kufanya hivyo hudai kujikana. Lakini kwa namna fulani wanajishawishi kwamba kuna faida ya kusikiliza mahubiri yenye kuwashtaki hivyo, hata kama watarekebisha maisha yao au hapana. Yakobo alionya dhidi ya kitu hicho hicho, hivi: “Lakini iweni watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu, hali mkijidanganya nafsi zenu” (Yakobo 1:22).
Wasikiaji ambao si watendaji wanajidanganya kwa sababu wanafikiri wameokoka, kumbe sivyo. Aina hiyo ya wanaojiita Wakristo ni tatizo kubwa kwa wachungaji wengi wanaompenda Mungu, wanaoshangazwa na jambo moja: mbona watu katika makanisa yao hawabadiliki wala kuonyesha hatua zozote za kukua kuelekea kwenye utakatifu? Sababu ni kwamba hao watu hawajawahi kujitia nira ya Yesu na hawajawahi kuzaliwa mara ya pili. Wanaweza kufikiri kwamba wamezaliwa mara ya pili kwa sababu kuna wakati waliwahi kuomba sala ya wokovu na sasa wanaelewa kwamba wokovu ni kwa neema, si kwa matendo. Lakini hawajaokoka kwa sababu hawajajitoa kuwa chini ya mamlaka ya Yesu. Juhudi zozote za kuwafanya watu kutenda kama Kristo zitakuwa bure mpaka wachukue hatua hiyo ya kwanza.
Msingi wa utakaso ni kujitoa kwa Mungu; utakaso hautatokea kwa mtu yeyote bila ya kunyenyekea kwanza. Lakini, tukisha jitoa na kunyenyekea, utakaso unaendelea maishani mwetu kadiri tunavyojifunza mapenzi ya Mungu na kweli za kiroho. Kwanza tunajitia nira ya Yesu; kisha tunajifunza “kwake” kama alivyosema Mwenyewe (Mathayo 11:29). Tunakua “katika neema na kumjua Bwana wetu na Mwokozi Yesu Kristo” (2Petro 3:18 – Maneno mepesi kutilia mkazo).
Mwanzoni, hatujui kikamilifu mapenzi ya Mungu au kila kitu ambacho ametutendea kwa njia ya Kristo, wala hatutambui kila kitu kinachohitaji kubadilishwa katika maisha yetu. Lakini, kama Paulo alivyoandika, tuna”jitahidi kujifunza kile kinachompendeza Bwana” (Waefeso 5:10). Hii ndiyo sababu maombi ya Paulo kwa Wakristo ni sala kwamba waongezeke katika ufahamu wa kiroho na maarifa. Na ndiyo sababu mara nyingi Paulo aliwashauri wasomaji wake akitumia maneno haya: “Au hamjui ya kuwa …?” Alitazamia kwamba waamini aliokuwa anawaandikia wangetenda kitofauti kama wangejua kweli fulani za kimungu, kama vile kwamba miili yao ni hekalu la Roho Mtakatifu.
Hii ndiyo sababu ni muhimu sana kwa wafuasi wa Kristo kujipatia kila kitu ambacho Mungu amekitoa kwao ili wajifunze kweli za kiroho. Wanatakiwa kujifunza Maandiko wao wenyewe, na wafuasi wa kweli wa Kristo watafanya hivyo kwa sababu wana shauku ya kutaka kujifunza mambo ya kiroho. Wanapaswa wajitoe kwa ajili ya mafundisho kanisani kutoka kwa wale ambao Mungu amewaita kufundisha Neno Lake. Wanapaswa kuwa sehemu ya kanisa la mahali, lenye maono ya kufanya wafuasi. Hayo ndiyo anayotaka Yesu. Alisema, “Basi enendeni mkawafanye … wote kuwa wanafunzi … mkiwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi” (Mathayo 28:19-20). Wanafunzi wa kweli wanajifunza.
Kusonga Mbele Kufikia Ukamilifu
Paulo aliandika hivi katika barua yake ya pili kwa Wakorintho: “Basi wapenzi wangu, kwa kuwa tuna ahadi hizo, na tujitakase nafsi zetu na uchafu wote wa mwili na roho, huku tukitimiza utakatifu katika kumcha Mungu” (2Wakor. 7:1). Hii inatuonyesha sisi kwamba waamini wa kweli si wakamilifu, kama inavyodaiwa na watu wenye msimamo mkali. Kuchafuka kimwili na kiroho huwa sehemu ya maisha ya waamini wa kweli. Lakini, lazima tusome maneno ya Paulo katika mantiki ya Agano Jipya. Japo Wakristo wa kweli wanaweza kunajisika kidogo, wao wanahesabiwa katika haki kwa sehemu kubwa. Ona kwamba Paulo hakuwashauri wasomaji wake waanze kutenda kama watakatifu. Badala yake, aliwashauri wao kutimiza utakatifu wao. Unaweza kutimiza kile ambacho tayari unakifanya vizuri. Maneno ya Paulo yanaonyesha kwamba Wakristo Wakorintho tayari walikuwa wanatenda kitakatifu, na wakati huo utakatifu wao ulihitaji kukamilishwa. Huo ndiyo utakaso Kibiblia – kukamilisha au kutimiza utakatifu.
Maneno ya Paulo pia yanatusaidia kuelewa kwamba mpango huo unaoendelea wa utakaso maishani mwetu si kitu ambacho Mungu anafanya bila sisi. Ni lazima sisi tujitakase kutokana na uchafu wa kimwili na unajisi wa kiroho. Mwandishi wa Waebrania anasema, “Tafuteni sana … huo utakatifu ambao hapana mtu atakayemwona Mungu asipokuwa nao” (Waebrania 12:14). Mungu haweki kando hiari yetu, na Maandiko yanasema wazi sana juu ya wajibu wetu katika mpango wa utakaso.
Lakini kwa upande wa pili, tusije tukafikiri kwamba utakaso ni kitu tunachopaswa kufanya mbali na kuhusika kwa Mungu. Paulo pia aliandika hivi: “Nami niliaminilo ndilo hili, ya kwamba Yeye aliyeanzisha kazi njema mioyoni mwenu ataimaliza hata siku ya Kristo Yesu” (Wafilipi 1:6). Pengine, wajibu wetu na wajibu wa Mungu unaelezwa vizuri sana katika Wafilipi 2:12-13, kama anavyoandika Paulo, hivi:
Basi wapendwa wangu, kama vile mlivyotii sikuzote, si wakati mimi nilipokuwapo tu, bali sasa zaidi sana mimi nisipokuwapo, utimizeni wokovu wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka. Kwa maana ndiye Mungu atendaye kazi ndani yenu, kutaka kwenu na kutenda kwenu, kwa kulitimiza kusudi lake jema” (Maneno mepesi kutilia mkazo).
Paulo alikuwa anawaandikia waamini wa kweli, wale waliotii hata wakati yeye mwenyewe hayupo. Bila shaka Mungu alikuwa anatenda kazi ndani yao kwa Roho Wake Mtakatifu, aliyekuwa ndani yao. Basi, walikuwa na wajibu mkubwa wa kushirikiana Naye katika kila alichokuwa anafanya maishani mwao. Utakaso hutokea wakati tunaposhirikiana na Mungu.
Hatua Za Utakaso
Katika sura hii na inayofuata, tutatazama hatua za utakaso, au jinsi utakaso unavyofanyika, na jinsi Mungu anavyohusika, na sisi pia. Hebu tuanze mwanzo kabisa.
Kazi ya Mungu ilianza muda mrefu sana kabla yeyote hajatakaswa. Yeye ndiye alipanga kabla mpango wa wokovu kupitia Mwana Wake, aliyetimiza mpango huo kwa kufa kwa ajili ya dhambi zetu na kufufuka kutoka kwa wafu. Kwa njia ya mjumbe aliyetumwa na Mungu anayehubiri Injili, na kwa nguvu za kushawishi za Roho Mtakatifu, mwenye dhambi huamshwa na kuhukumiwa juu ya dhambi zake na kujisikia hitaji la wokovu.
Hapo kwenye kuokoka ndipo wajibu wa mwanadamu huingia. Tuna uchaguzi, na itikio la pekee linalofaa kwa upande wetu ni kutubu dhambi zetu na kumwamini Yesu. Mungu anatuagiza tutubu na kumwamini Yesu, kwa hiyo, kutubu na kuamini lazima kuwa wajibu wetu pia – si wa Mungu.
Lakini – mara tunapotubu na kuiamini Injili, Mungu anaingia kazini tena. Mara moja anakaa ndani yetu kwa njia ya Roho Mtakatifu, akihuisha roho zetu na kuvunja nguvu za dhambi maishani mwetu, na kutuweka huru kutokana na vifungo vyake. Roho zetu zinazaliwa upya, zinaumbwa tena katika sura ya Kristo, nasi tunafanyika viumbe vipya ndani Yake (ona 1Petro 1:3; Waefeso 4:24; 2Wakor. 5:17). Mungu anakuwa Baba yetu kiroho.
Matokeo ni kiwango fulani cha utakatifu mara moja, kinachodhihirika katika maisha ya mwamini mpya. Kutokana na maandiko kama 1Wakor. 6:9-10; Wagalatia 5:19-21; Waefeso 5:5-6; 1Yohana 3:15 na Ufunuo 21:8, ni hakika kwamba kuzaliwa upya hukomesha zile tabia za kawaida za dhambi mbaya sana kama vile uzinzi, uasherati, uchafu, ufisadi, tamaa, ulawiti, ashiki, wizi, kudhulumu, ulevi, fujo, matukano, uadui, ugomvi, wivu, hasira, faraka, fitina, kuabudu sanamu, uchawi, kuua na uongo.
Hii haimaanishi kwamba mwamini wa kweli hawezi kutenda dhambi hizo. Mwamini yeyote anaweza, akitaka, kutenda dhambi hizo, kwa sababu Mungu hajamwondolea hiari yake. Lakini, atagundua kwamba ndani yake kuna upinzani na hali ya kuchukia dhambi ambayo haikuwepo kabla. Uwezo wake wa kupinga majaribu unaongezeka sana. Kama atakubali majaribu, atajisikia kuhukumiwa sana na mwenye huzuni mpaka atubu dhambi yake kwa Mungu. Hapa tena niseme, kama Maandiko yanavyotuonya sana – kutenda dhambi kama hizo ni uhakikisho kwamba mtu hataurithi ufalme wa Mungu.
Je, Dhambi Zote Ni Sawa Machoni Pa Mungu?
Kuna watakaosema kwamba “dhambi zote ni sawa” na kwa sababu hiyo, kutenda bila kutubu dhambi zote hizo zinazotajwa hapo juu si tofauti na kutenda bila kutubu dhambi zingine zozote. Lakini, hoja hii haibadilishi Maandiko tuliyokwisha yataja, wala haitii nguvu upinzani wa aina yoyote kinyume cha niliyokwisha sema. Kama dhambi zote ni sawa mbele za Mungu, basi lazima tuipanue sana ile orodha ya Paulo ya dhambi na kuweka kila dhambi, na kuamua kwamba hakuna mtu aliyeokoka! Lakini, kwa neema – kutokuwa na shukrani, wasiwasi na kusinzia wakati wa mahubiri havijatajwa katika orodha yoyote ya Paulo!
Basi, dhambi hazifanani mbele za Mungu. Yesu alizungumza kuhusu amri ndogo na kubwa (ona Mathayo 5:19). Alizungumza juu ya “dhambi kuu” na dhambi ndogo (ona Yohana 19:11). Aliihesabu amri moja kuwa “kuu, na ya kwanza” (Mathayo 22:38), na nyingine kuwa ya pili. Alitaja juu ya dhambi moja ambayo haisameheki kabisa (ona Mathayo 12:31-32). Aliwakemea Mafarisayo, ambao walipuuza “mambo makuu ya sheria, yaani: adili, na rehema, na imani,” na kutilia mkazo matakwa yale madogo madogo ya sheria kama vile kutoa zaka (Mathayo 23:23 – Maneno mepesi ni kutilia mkazo).
Ukweli kwamba dhambi fulani ni mbaya sana mbele za Mungu kuliko zingine unaonekana katika Torati ya Musa, ambamo makosa fulani yalidai adhabu kali sana. Pia tunaona kwamba Mungu aliwapa Israeli amri kumi kwanza badala ya kumi na moja au arobaini. Hii ilionyesha kwamba anazihesabu amri zingine kuwa muhimu kuliko zingine.
Tunasoma katika Ezekieli sura ya 8 jinsi Bwana alivyomwonyesha picha nne za dhambi fulani zinazotendwa Israeli. Kila iliyofuata Mungu aliitaja kuwa “chukizo zaidi” kuliko iliyokuwa imetangulia.
Mtume Yohana alisema kwamba ipo dhambi “isiyo ya mauti” na nyingine “ya mauti” (1Yohana 5:16-17).
Basi, dhambi hazifanani mbele za Mungu. Ni kweli kwamba dhambi zote hututenganisha na Mungu, na dhambi zote humhuzunisha Mungu, lakini si zote zenye kulingana katika kumhuzunisha. Kila mtu anajua kwamba kuua na kumpiga mtu konde ni makosa. Lakini pia, kila mtu anajua kwamba kosa la kwanza ni baya na kubwa kuliko lile la pili.
Badiliko La Kwanza Na Linaloendelea
Kama umezaliwa mara ya pili, Mungu amekwisha shughulika na kile kinachomwudhi zaidi. Umepata mabadiliko. Lakini Mungu hatosheki na hicho tu. Lengo Lake kwa ajili yako wewe ni ukamilifu – basi, utazamie mabadiliko yanayoendelea kutokea. Ni hivi:
Insert Chart here:
Wanadamu wote wamegawanywa katika makundi mawili: waliookoka na wasiookoka. Hakuna wengine hapo katikati. Unakuwepo katika kundi moja au la pili.
Unapotoka upande mmoja kuelekea ule mwingine, unapiga hatua kutoka kwenye uovu na kwenda kwenye utakatifu. Upande wa WASIOOKOKA una wale watu ambao ni waovu kabisa na wale ambao si waovu sana. Si watu wote wasiookoka ambao ni waovu sana.
Lakini, unapozidi kusogea kuelekea utakatifu, utavuka mstari ambao ni mfano wa kuokoka na kuzaliwa upya. Mara tu ukisha pita mstari huo, wewe umeingia katika waliookoka. Ila, katika waliookoka wapo ambao si watakatifu sana, na ambao wamepiga hatua katika utakatifu. Si wote waliookoka ambao ni watakatifu kabisa.
Lakini, tofauti inayoletwa na mtu kupita mstari wa kuokoka ni kubwa, ndiyo maana hakuna “eneo la katikati”. Mtume Yohana aliandika kwamba waliookoka na wasiookoka ni dhahiri (ona 1Yohana 3:10).
Kadiri mtu aliyeokoka anavyotakaswa kwa kushirikiana na Roho Mtakatifu, anaendelea kusogea kwenye eneo la UKAMILIFU. Ila kwa wakati huu, Mungu tu ndiye mkamilifu.
Tunapozaliwa mara ya pili tu, Mungu anafanikisha kazi Yake inayoendelea ya kutubadilisha kwa kutumia njia mbalimbali ambazo tutazitazama. Lakini kwanza inatubidi tuelewe kwamba mafanikio ya Mungu yanategemea sana ushirikiano wetu. Yeye haweki kando hiari yetu. Ila pia, anatoa vivutio vingi na kutuwezesha kushirikana Naye.
Je, ni kitu gani kinachotuhamasisha tupambane na dhambi na kuzidi kufanana na Yesu? Kuna vitu vitatu ambavyo Mungu anatupa sisi: upendo, tumaini na hofu. Vyote hivyo ni halali, na vinalingana na Maandiko. Kwa upana zaidi, ni (1) upendo kwa Mungu, (2) tumaini la kupata thawabu, na (3) hofu ya kupata adhabu.
Upendo Kwa Mungu
Utii utokanao na upendo unaonekana kuwa aina ya utii ya hali ya juu sana, yenye kumpendeza Mungu. Kwa kweli tunapaswa kumtii Yeye kwa sababu tunampenda, na kila mwamini wa kweli atafanya hivyo kiasi fulani. Yesu alizungumza juu ya utii wa upendo, hivi:
“Mkinipenda, mtazishika amri zangu … Yeye aliye na amri zangu na kuzishika, yeye ndiye anipendaye; naye anipendaye atapendwa na Baba yangu; nami nitampenda na kujidhihirisha kwake” (Yohana 14:15, 21).
Naye mtume Yohana aliandika hivi:
Kwa maana huku ndiko kumpenda Mungu, kwamba tuzishike amri zake; wala amri zake si nzito (1Yohana 5:3).
Tunawezaje kuacha kumpenda wakati tunapoelewa kile alichotutendea? Tunawezaje kutokuwa na shukrani kwa kujikana Kwake kwa hali ya juu, kwa ajili yetu? Tunawezaje kuacha kutafuta kumpendeza Yeye, atupendaye sisi sana?
Hebu tufikiri tu kwamba unavuka barabara yenye magari mengi sana kwenye kona, na ghafula unatokezea mbele ya basi kubwa linalokuja kasi. Mtembea miguu mwenzako anajitahidi kukusukuma, na anafanikiwa kukuondoa katika hatari, lakini yeye mwenyewe anagongwa na basi hilo. Anakimbizwa hospitali haraka, na huko anagundua kwamba hataweza tena kutembea, bali atategemea kiti cha magurudumu maisha yake yote.
Je, wewe hutajisikia deni la shukrani kwa mtu ambaye ameokoa maisha yako kwa gharama kubwa hivyo? Je, hutajisikia wajibu wa kulipa kitu ambacho hata huwezi kukilipia? Upendo wako kwa yule aliyekuonyesha upendo mkubwa hivyo ungekuhamasisha ufanye chochote uwezacho ili kumpendeza. Kama angetaka kitu, ungefanya juu chini ili umpe. Ndivyo ilivyo kwa wale wanaomwamini Yesu. Hawana jinsi – lazima wampende, na kwa sababu wanampenda, wanajitahidi sana kumpendeza kwa utii wao.
Tumaini La Kupata Thawabu
Hamasisho la pili ambalo Mungu huwapa wale wanaomtii ni tumaini la kupata thawabu. Kweli, tunapata wokovu kwa neema ya Mungu. Lakini hiyo si kusema kwamba baraka zingine hazipatikani kwa matendo yetu. Baraka za sasa na za baadaye zimeahidiwa katika Maandiko kwamba ni thawabu kwa watii. Paulo aliandika hivi: “Utauwa hufaa kwa mambo yote; yaani, unayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye"”(1Timo. 4:8). Kweli, Mungu “huwapa thawabu wale wamtafutao kwa bidii” (Waebrania 11:6).
Tumaini la kupata thawabu linaweza kuonekana kama jambo la ubinafsi na uchoyo. Si la maana ukilinganisha na kuhamasishwa na kumpenda Mungu. Je, Bwana si angependa kwamba tumtumikie kwa kuwa tunampenda, badala ya kufanya hivyo kwa sababu ya faida ya kibinafsi? (Kweli hiyo inaonyeshwa vizuri sana katika kujaribiwa kwa Ayubu!)
Nafikiri ni hivyo. Lakini, Mungu ndiye aliyeanzisha mpango huo wa kutoa thawabu kwa sababu ya utii. Kama mzazi yeyote mzuri, anaweza kupenda kwamba watoto Wake wamtii wakihamasishwa na pendo safi, lakini anajua, kama mzazi mzuri, kwamba upendo wa familia wakati mwingine hautoshi. Wazazi mara nyingi huwaahidi watoto wao tuzo kwa sababu ya tabia nzuri, na inafaulu. Tena, thawabu za kidunia tunazopokea hutukuza uzuri na wema wa Mungu wetu ambaye anapenda kuwabariki watoto Wake.
Pia, lazima tukumbuke kwamba uchoyo ni kujitumikia wenyewe huku wengine wakipata shida. Basi, si kila kitu kinachofaidia kilicho kibaya. Bila ya kukemea chochote, Maandiko yanawaeleza Wakristo wa kweli kwamba ni wale ambao “kwa saburi katika kutenda mema hutafuta utukufu na heshima na umilele” (Warumi 2:7 – Maneno mepesi ni kutilia mkazo). Nadhani wengi wetu tulimwamini Kristo kwa sababu ya kujijali – tunataka kwenda mbinguni, tusiende jehanamu. Lakini, tendo letu la kumwamini Kristo lisihesabiwe kwamba ni la kibinafsi na uchoyo. Sisi kupokea uzima wa milele hakumzuii mtu yeyote kupokea huo uzima. Sana sana ni kwamba kupokea kwetu uzima wa milele kuliongeza uwezekano wa wengine kuokoka pia. Basi, kupokea wokovu kwa sababu ya kujijali si kitu cha kichoyo. Na ndivyo ilivyo kuhusu thawabu ambazo Mungu ameahidi kwa watauwa. Haziji na kuwafanya wengine wazikose. Tena neema ya Mungu na thawabu Zake hazimaliziki. Si kwamba tunashindana na wengine kwamba nani atapata kipande na mwingine akose.
Basi kama ni hivyo, shauku ya kupata thawabu isionekane kuwa dhambi, au makosa, au uchoyo, hasa kwa sababu mwanzilishi na mwenye kuahidi thawabu hizo ni Mungu. Kama ingekuwa ni kosa kwetu kutamani thawabu ambayo Mungu ameahidi, basi Yeye ndiye mwenye makosa kwa kutushawishi tufanye kosa. Jambo hilo linamfanya Yeye kuwa mwenye dhambi, kitu ambacho hakiwezi kutokea kamwe!
Malipo Sawasawa Na Matendo
Katika Maandiko, watauwa wanaahidiwa thawabu maalum kwa ajili ya kutii kwao. Kwa mfano: Tunajua kwamba katika ufalme ujao wakati Kristo atakaporudi, Mungu atamlipa kila mmoja wetu kulingana na matendo yake.
“Kwa sababu Mwana wa Adamu atakuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika zake; ndipo atakapomlipa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake” (Mathayo 16:27 – Maneno mepesi kutilia mkazo).
“Tazama. Naja upesi, na ujira wangu u pamoja nami, kumlipa kila mtu kama kazi yake ilivyo” (Ufunuo 22:12 – Maneno mepesi kutilia mkazo).
Thawabu na ujira ambazo Yesu anazungumzia, si tu kwamba ni malipo ya jumla ambayo wote waliookoka au wasiookoka watayashiriki pamoja – yaani mbinguni au jehanamu. Malipo na ujira vilvyoahidiwa pia ni thawabu maalum na za kibinafsi ambazo zinatokana na matendo ya kila mtu kibinafsi. Paulo, akiandika kuhusu huduma yake na ya Apolo, anasema hivi:
Basi yeye apandaye na yeye atiaye maji ni wamoja, lakini kila mtu atapata thawabu yake mwenyewe sawasawa na taabu yake mwenyewe (1Wakor. 3:8 – Maneno mepesi ni kutilia mkazo. Ona pia ms. 9-15).
Thawabu zetu wakati ujao misingi yake itakuwa ni matendo yetu wenyewe. Hii itatokana na karama zetu binafsi, vipawa na uwezo, na nafasi zilizopatikana. Mfano aliotoa Yesu wa Talanta unaliweka hilo wazi zaidi (ona Mathayo 25:14-30). Mungu anatazamia vingi kutoka kwa wale aliowapa vingi. Yesu alisema hivi, “Kwa maana, aliyepewa vingi, vingi vitatakiwa” (Luka 12:48).
Wakati Wa Thawabu Hizo
Maandiko hayaweki wazi kila wakati kwamba ni lini watauwa watapewa thawabu zao. Zipo ahadi ambazo ni kwa ajili ya wakati huu maishani, na zingine ni kwa ajili ya baadaye. Zingine hazieleweki. Basi, hebu kwanza tutazame zile chache ambazo zinaonyesha thawabu katika maisha haya:
Waheshimu baba yako na mama yako; amri hii ndiyo amri ya kwanza yenye ahadi, upate heri, ukae siku nyingi katika dunia (Waefeso 6:2-3. Maneno mepesi kutilia mkazo).
“Msihukumu, nanyi hamtahukumiwa. Msilaumu, nanyi hamtalaumiwa. Achilieni, nanyi mtaachiliwa. Wapeni watu vitu nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa na kusukwa-sukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa” (Luka 6:37, 38 – Maneno mepesi kutilia mkazo).
“Kwa maana, ‘Atakaye kupenda maisha na kuona siku njema, auzuie ulimi wake usinene mabaya na midomo yake isiseme hila’.” (1Petro 3:10 – Maneno mepesi kutilia mkazo)
Lakini aliyeitazama sheria kikamilifu iliyo ya uhuru na kukaa humo, asiwe msikiaji msahaulifu bali mtendaji wa kazi, huyo atakuwa heri katika kutenda kwake (Yakobo 1:25 – Maneno mepesi kutilia mkazo).
Ifuatayo ni mifano michache ya ahadi ambayo ni dhahiri kwamba inahusu wakati wa maisha yetu yajayo.
“Bali ufanyapo karamu waite maskini, vilema, viwete, vipofu, nawe utakuwa heri, kwa kuwa hao hawana cha kukulipa; kwa maana utalipwa katika ufufuo wa wenye haki” (Luka 14:13, 14 – Maneno mepesi kutilia mkazo).
”Furahini na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana ndivyo walivyowaudhi manabii waliokuwa kabla yenu” (Mathayo 5:12 – Maneno mepesi kutilia mkazo).
“Viuzeni mlivyo navyo mtoe sadaka. Jifanyieni mifuko isiyochakaa, akiba isiyopungua katika mbingu, mahali pasipokaribia mwivi, wala nondo haharibu” (Luka 12:33 – Maneno mepesi kutilia mkazo).
Kwamba ni thawabu gani za kimbinguni zinazotusubiri, Mungu tu ndiye ajuaye. Pamoja na kwamba mbinguni si mahali tunapojua sana, hata thawabu zinazotusubiri huko ni hivyo. Lakini, zile za hapa duniani zieleweke kwamba ni chochote tunachoweza kuhesabu kwamba ni baraka. Usimwekee mipaka Mungu kwa kusema baraka Zake ni kujisikia vizuri tu ndani ya moyo au kusisimka mpaka unasikia kuwashwa katika mgongo wako!
Mwisho: Baadhi ya ahadi ambazo muda wake wa kupewa thawabu haujulikani ni kama hizi.
“Bali wapendeni adui zenu, tendeni mema na kukopesha msitumaini kupata malipo, na thawabu yenu itakuwa nyingi; nanyi mtakuwa wana wa Aliye juu, kwa kuwa yeye ni mwema kwa wasiomshukuru, na waovu” (Luka 6:35 – Maneno mepesi ni kutilia mkazo).
“Bali wewe utoapo sadaka, hata mkono wako wa kushoto usijue ufanyalo mkono wako wa kuume; sadaka yako iwe siri; na Baba yako aonaye sirini atakujazi … Bali wewe usalipo, ingia katika chumba chako cha ndani, na ukiisha kufunga mlango wako, usali mbele za Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi … Bali wewe ufungapo, jipake mafuta kichwani, unawe uso; ili usionekane na watu kuwa unafunga ila na Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi” (Mathayo 6:3-4; 6; 17-18. Maneno mepesi ni kutilia mkazo).
Kwa nia njema kama kumtumikia Bwana wala si mwanadamu; mkijua ya kuwa kila neno jema alitendalo mtu atapewa lilo hilo na Bwana, kwamba ni mtumwa au kwamba ni huru (Waefeso 6:7, 8 – Maneno mepesi ni kutilia mkazo).
Mungu anafuatilia hata tendo jema lililo dogo sana, akiwa na mpango wa kutoa thawabu kwa ajili yake.
“Kwa kuwa yeyote atakayewanywesha ninyi kikombe cha maji kwa kuwa ninyi ni watu wa Kristo, amin nawaambia, hatakosa thawabu yake” (Marko 9:41).
Je, ungependa kufurahia baraka zaidi kutoka kwa Baba yako wa mbinguni, sasa na baadaye huko mbinguni? Bila shaka unapenda hivyo! Basi, mtii zaidi, nawe utapata thawabu. Yesu alisema hivi: “Heri walisikiao neno la Mungu na kulishika” (Luka 11:28 – Maneno mepesi kutilia mkazo).
Hofu Ya Kuadhibiwa
Ukiondoa upendo kwa Mungu na tumaini la kupata thawabu, kuna njia nyingine moja ambayo Mungu anaitumia kuwahamasisha watoto Wake kutii: kwa njia ya kuogopa adhabu. Nadhani kwamba katika njia hizo tatu, hii ndiyo asiyopenda kuitumia sana. Lakini, ni kitu halisi na kukubalika na Maandiko. Wazazi wengi hutumia njia zote hizo tatu kuwahamasisha watoto wao watii, na hakuna hata moja inayostahili kulaumiwa.
Kuna wanaotoa hoja kupinga hii njia kwamba kumhofu Mungu ni kitu kisicholingana na kumpenda. Kwani Maandiko hayasemi kwamba “pendo la kweli hufukuza nje hofu” (1Yohana 4:18)?
Hofu ambayo Yohana aliandika juu yake inayofukuzwa na pendo sio hofu ya kumcha Mungu kwa utakatifu. Ni hofu ya hukumu ya milele ambayo inaanza “siku ya hukumu” (1Yohana 4:17). Baada ya kuelewa na kuupokea upendo wa Mungu, na kwa kuwa sasa tunadumu katika pendo Lake (ona Yohana 15:10), hatuna haja ya kuogopa ile jehanamu ambayo tulikuwa tunaistahili hapo kwanza.
Kumpenda na kumhofu Mungu ni vitu vinavyokwenda pamoja, kulingana na Agano Jipya. Waamini wanaagizwa kumhofu Mungu (ona 1Petro 2:17). Wanaambiwa kunyenyekeana wao kwa wao “katika hofu ya Kristo” (Waefeso 5:21), “kuutimiza wokovu kwa hofu na kutetemeka” (Wafilipi 2:12), na kuukamilisha utakatifu wao “katika hofu ya Mungu” (2Wakor. 7:1). Petro aliwashauri wale waliopokea barua yake ya kwanza waenende kwa hofu katika safari yao hapa duniani, wakijua kwamba Mungu angewahukumu kila mmoja wao bila upendeleo, kulingana na matendo yao (ona 1Petro 1:17).
Adhabu Huko Korintho
Kwa bahati mbaya sana, adhabu ya Mungu ni wazo geni kabisa kwa wengi wanaojiita Wakristo, japo si geni katika Biblia. Adhabu ya Mungu inadhihirishwa katika Maandiko tangu Adamu na Hawa hadi Anania na Safira. Inadhihirishwa tangu Waisraeli waliokufa nyikani hadi Wakristo waliokuwa wagonjwa huko Korintho. Wakati mwingine adhabu Yake inaweza kuwa kali sana wakati kuna sababu nzuri. Hebu fikiri maneno muhimu sana ya Paulo kwa Wakorintho, anaposema hivi:
Basi kila aulaye mkate huo, au kukinywea kikombe hicho cha Bwana isivyostahili, atakuwa amejipatia hatia ya mwili na damu ya Bwana. Lakini mtu ajihoji mwenyewe, na hivyo aule mkate na kukinywea kikombe. Maana alaye na kunywa, hula na kunywa hukumu ya nafsi yake, kwa kutokuupambana ule mwili. Kwa sababu hiyo wako wengi kwenu walio hawawezi na dhaifu, na watu kadha wa kadha wamelala. Lakini kama tungejipambanua nafsi zetu, tusingehukumiwa. Ila tuhukumiwapo, twarudiwa na Bwana, isije ikatupasa adhabu pamoja na dunia (1Wakor. 11:27-32. Maneno mepesi kutilia mkazo)
Kwanza: Ona kwamba, kwa sababu ya adhabu ya Mungu ambayo Paulo anaiita hukumu pia, baadhi ya Wakorintho walikuwa dhaifu na wagonjwa. Wengine walikuwa wamekufa.
Sababu ya hukumu ya Mungu: Walikuwa wanashiriki Meza ya Bwana kwa “jinsi isivyostahili” (11:27). Paulo anamaanisha nini hapo? Kutokana na mantiki tunaweza kusema kwamba alikuwa anazungumzia kitendo cha kushiriki Meza ya Bwana huku wamemwasi Bwana. Kwa mfano: Paulo aliandika kwamba tunatakiwa kwanza tujipime (au tujihoji) sisi wenyewe kabla ya Meza ya Bwana, na akaonya kwamba tuko katika hatari ya kuhukumiwa kama hatuta”pambanua mwili ipasavyo” (11:29). Inaonekana kwamba huku “kuupambanua mwili” ni sawa na kujipima na kujihoji. Tunajua kwamba “matendo ya mwili” ndiyo yanayotuletea matatizo (ona Warumi 8:12-14; 1Wakor. 9:27). “Kuupambanua mwili” bila shaka maana yake ni kutambua na kuitiisha ile asili ya dhambi iliyo ndani yetu, yenye kufanya vita kila wakati na Roho. Tunaweza kuepuka hukumu ya Mungu kama tutajipima wenyewe – kujihukumu – yaani, kama tutakataa kukubaliana na ile asili yetu ya dhambi, na tujihoji kila mara na kutubu dhambi zetu kama inabidi kufanya hivyo.
Je, Walio-okoka Wanaweza Kwenda Jehanamu?
Kama Paulo anavyoandika, Mungu hutuadhibu “ili isitupase adhabu pamoja na dunia” (11:32). Dunia itahukumiwa kupotea milele. Basi, Mungu huwaadhibu waamini watendao dhambi ili wasiende jehanamu.
Hili linaleta maswali kadhaa ya muhimu. La kwanza ni hili: Je, kweli ipo hatari ya mwamini wa kweli kufika jehanamu?
Jibu ni NDIYO. Kama mwamini wa kweli atarudia kutenda zile “dhambi zinazotenganisha” – yaani, zile ambazo Maandiko yanasema zikitendwa, mtu hataweza kuingia katika ufalme wa Mungu (ona 1Wakor. 5:11; 6:9-10; Wagalatia 5:19-21; Waefeso 5:5, 6). Anapoteza uzima wa milele. Mungu hajaondoa hiari yetu, wala uwezo wetu wa kufanya dhambi. Kinyume na jinsi waalimu wengi wa siku hizi wanavyofundisha, Biblia inafundisha kwamba mwamini yeyote atakayefuata asili yake ya kale ya dhambi – au mwili – yuko katika hatari ya kufa kiroho. Paulo anasema hivi, anapowaandikia Wakristo:
Basi kama ni hivyo ndugu, tu wadeni, si wa mwili tuishi kwa kufuata mambo ya mwili. Kwa maana, kama tukiishi kwa kufuata mambo ya mwili, mwataka kufa; bali kama mkiyafisha matendo ya mwili kwa Roho, mtaishi. Kwa kuwa wote wanao-ongozwa na Roho wa Mungu, hao ndio wana wa Mungu (Warumi 8:12-14. Maneno mepesi kutilia mkazo).
Inatubidi tuseme kwamba Paulo alikuwa anasema na waamini Wakristo walio hai kiroho, kwa sababu mbili.
Kwanza: Ona kwamba anawaita ndugu.
Pili: Walikuwa na uwezo wa kuyafisha matendo ya mwili kwa njia ya Roho. Hiki ni kitu ambacho waamini tu wanaweza kukifanya, ambao Roho wa Mungu anakaa ndani yao.
Ona sasa kwamba Paulo aliwaonya Wakristo Warumi kwamba, kama wangeishi kulingana na mwili, ni lazima wafe. Je, alikuwa anazungumza juu ya kifo cha kimwili au cha kiroho? Ni sahihi tukisema kwamba alikuwa anazungumzia juu ya kifo cha kiroho kwa sababu, kila mmoja – hata wale wenye “kuyafisha matendo ya mwili” – watakufa kimwili siku moja. Je, si kweli kwamba wale “wanaoishi kwa kuufuata mwili” mara nyingi huendelea kuishi katika mwili kwa muda mrefu tu?
Uamuzi tunaoweza kufikia kutokana na kweli hizi ni kwamba waamini Wakristo wanaweza kufa kiroho kwa “kuishi kwa kuufuata mwili”. Basi, zile orodha za “dhambi” za Paulo katika 1Wakor. 6:9-10; Wagalatia 5:19-21 na Waefeso 5:5-6 hazipaswi kufikiriwa kwamba zinawahusu wale tu wasiokiri kumwamini Kristo. Zinawahusu hata wale ambao wamekiri kumwamini Kristo. Ukweli ni kwamba, katika mantiki yake, zile dhambi ziliandikwa ili kuwa maonyo kwa waamini. NI wale wanao-ongozwa na Roho badala ya mwili ndiyo walio wana wa kweli wa Mungu, kama Paulo alivyosema waziwazi kabisa (ona Warumi 8:14).
Uthibitisho Zaidi Kwamba Walio-Okoka Wanaweza Kufa Kiroho
Paulo aliandika maneno kama hayo kwa Wakristo Wagalatia. Baada ya kuwaonya kwamba wale wanaojihusisha na “matendo ya mwili” hawataurithi ufalme wa Mungu, alisema hivi:
Msidanganyike. Mungu hadhihakiwi; kwa kuwa chochote apandacho mtu, ndicho atakachovuna. Maana yeye apandaye kwa mwili wake, katika mwili wake atavuna uharibifu; bali yeye apandaye kwa Roho, katika Roho atavuna uzima wa milele. Tena tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho (Wagalatia 6:7-9. Maneno mepesi kutilia mkazo).
Ona hapo kwamba watu wawili wanatofautishwa. Mmoja anapanda kwa mwili wake na mwingine kwa Roho. Wa kwanza anavuna uharibifu na wa pili anavuna uzima wa milele. Kama uharibifu ndicho kinyume cha uzima wa milele, basi bila shaka maana yake nyingine ni kifo cha kiroho. Ona hapa kwamba kuvuna uzima wa milele kunaahidiwa kwa wale tu wanaopanda kwa Roho, na wanaoendelea kupanda kwa Roho. Wale wanaopanda kwa mwili hawatavuna uzima wa milele bali uharibifu. Kama Paulo alivyotoa onyo, “Msidanganyike” kuhusu hilo! (Wagalatia 6:7). Lakini, wengi sana wamedanganyika siku hizi.
Kupanda kwa mwili ni kitu kilichomkera sana mtume Paulo, ambaye, kama Mkristo mwingine yeyote wa kweli, bado alikuwa na asili ya dhambi. Aliwaandikia Wakorintho kama ifuatavyo:
Na kila ashindanaye katika michezo hujizuia katika yote. Basi hao hufanya hivyo kusudi wapokee taji iharibikayo; bali sisi tupokee taji isiyoharibika. Hata mimi napiga mbio vivyo hivyo, si kama asitaye; napigana ngumi vivyo hivyo, si kama apigaye hewa; bali nautesa mwili wangu na kuutumikisha; isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine, mwenyewe niwe mtu wa kukataliwa (1Wakor. 9:25-27. Maneno mepesi kutilia mkazo)
Sawa na wanariadha wa Olimpiki, sisi pia lazima tuwe na kiasi kama tunatazamia kupokea zawadi yetu isiyoharibika. Paulo anataja kwamba aliutesa mwili wake na kuufanya mtumwa wake, kwa sababu kama asingefanya hivyo, alikuwa katika hatari ya “kukataliwa”. Mtu anapokataliwa, hakuna tumaini kwamba atashinda. Mantiki ya maneno ya Paulo yanaweka wazi kwamba yeye hakuwa na wasiwasi juu ya kupoteza nafasi zingine za baadaye kufanya huduma, au thawabu za mbinguni, bali kupoteza kabisa wokovu wake. Katika mistari inayofuata (1Wakor. 10:1-4) Paulo aliwaonya Wakristo Wakorintho wasifuate mfano mbaya wa Waisraeli, ambao, ingawa hapo kwanza walikuwa wamebarikiwa sana na kuwa na fursa nyingi, waliangamia nyikani baadaye kwa sababu hawakuendelea katika utii wa imani. Tofauti na Waisraeli walioangamia, waamini wa Korintho waliambiwa wakimbie choyo, kuabudu sanamu, uchafu (ambazo ni dhambi alizotaja Paulo katika orodha yake ya 6:9-10), kumjaribu Mungu na kunung’unika. Pia aliongeza ushauri huu: “Kwa hiyo, anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke” (1Wakor. 10:12).
Yakobo Anaongezea “Amina” Yake
Fikiri vile vile kile ambacho Yakobo aliwaandikia waamini Wakristo kuhusu kuvumilia wakati wa dhiki au majaribu. Wale wanaofaulu kufanya hivyo ndiyo watakaopokea “taji ya uzima” – yaani, wokovu. Wale watakaorudi kwenye tabia ya kutenda dhambi watakufa.
Heri mtu astahimiliye majaribu; kwa sababu akiisha kukubaliwa ataipokea taji ya uzima, Bwana aliyowaahidia wampendao. Mtu ajaribiwapo asiseme, Ninajaribiwa na Mungu; maana Mungu hawezi kujaribiwa na maovu, wala yeye mwenyewe hamjaribu mtu. Lakini kila mmoja hujaribiwa na tamaa yake mwenyewe huku akivutwa na kudanganywa. Halafu ile tamaa ikiisha kuchukua mimba huzaa dhambi, na ile dhambi ikiisha kukomaa huzaa mauti. Ndugu zangu wapenzi, msidanganyike (Yakobo 1:12-16. Maneno mepesi kutilia mkazo.)
Yakobo alisema kwamba si Mungu anayetujaribu, bali “kila mmoja hujaribiwa na tamaa yake mwenyewe huku akivutwa na kudanganywa” (1:14). Matokeo ni kwamba “tamaa ikiisha kuchukua mimba huzaa dhambi” (1:15). Mwishoni, ile dhambi “ikikomaa” huzaa mauti. Sasa: kwamba dhambi inachukua muda gani “kukomaa” ni swala la kutafiti, lakini, kwa hakika, dhambi moja inayotendwa na mwamini haimsababishii kufa kiroho wakati huo huo. Lakini, kuendelea katika dhambi, au kuzidi kuenenda katika matendo ya mwili mwisho wake ni kifo cha kiroho. Yakobo anatuonya kwamba tusidanganyike kuhusu hilo.
Hapa tena tunauliza: Inawezekanaje Yakobo awe anaonya juu ya kifo cha kimwili badala ya kifo cha kiroho, kama wengine wanavyosema? Wote watakufa kimwili wakati fulani, awe mwenye dhambi au mtakatifu.
Tena, wanawezaje watu wengine kusema kwamba Yakobo anazungumza na wasioamini katika maandiko haya? Haiwezekani dhambi “kuzaa mauti” kwao kwa sababu wao tayari “ni wafu katika dhambi na makosa yao” (Waefeso 2:1). Ni dhahiri kwamba Yakobo alikuwa anawaandikia Wakristo – “ndugu wapendwa” – kama tunavyoona katika Yakobo 1:16.
Halafu, mwishoni mwa barua yake aliandika hivi:
Ndugu zangu, ikiwa mtu wa kwenu amepotelea mbali na kweli, na mtu mwingine akamrejeza; jueni ya kuwa yeye amrejezaye mwenye dhambi hata atoke katika njia ya upotevu ataokoa roho na mauti, na kufunika wingi wa dhambi (Yakobo 5:19-20. Maneno mepesi kutilia mkazo)
Ona kwamba Yakobo alikuwa anazungumza na ndugu. Alisema kwamba ‘mtu wa kwenu akipotelea mbali na kweli.” Basi bila shaka alimaanisha waamini wengine ambao walikuwa katika kweli mwanzoni kisha wakapotea kutoka kwenye kweli hiyo. Yakobo kwa maneno yake anaonyesha kwamba hawakuwa wamepotea katika mafundisho tu, maana anasema, “yeye amrejezaye mwenye dhambi hata atoke katika njia ya upotevu” (5:20). Hao ni watu waliotoka kwenye utakatifu.
Lakini, tukimrudisha yule ambaye amepotea kama Yakobo alivyoeleza, tuta”okoa roho yake na mauti.” Angalia kwamba Yakobo hakusema tunaokoa mwili wake na mauti, bali alisema roho yake. Hapa tena, cha kutoa katika maneno ya Yakobo ni kwamba yeye aliamini kuwa mtu aliye hai kiroho angeweza kufa kiroho kwa kurudia matendo ya dhambi.
Petro Naye Anajiunga Hapa
Si Paulo na Yakobo tu waliokubaliana katika jambo hili. Hata Petro pia. Akionya juu ya kudanganywa kwa waamini na waalimu wa uongo, aliandika hivi:
Maana wakinena maneno makuu mno ya kiburi, kwa tamaa za mwili na kwa ufisadi huwahadaa watu walioanza kuwakimbia wale wanaoenenda katika udanganyifu; wakiwaahidia uhuru, nao wenyewe ni watumwa wa uharibifu. Maana mtu akishindwa na mtu huwa mtumwa wa mtu yule. Kwa maana wale waliokwisha kuyakimbia machafu ya dunia kwa kumjua Bwana na Mwokozi Yesu Kristo, kama wakinaswa tena na kushindwa, hali yao ya mwisho imekuwa mbaya kuliko ile ya kwanza. Maana ingekuwa heri kwao kama wasingaliijua njia ya haki kuliko kuijua kisha kuiacha ile amri takatifu waliyopewa. Lakini imetukia kwao sawasawa na ile mithali ya kweli, Mbwa ameyarudia matapiko yake mwenyewe, na nguruwe aliyeoshwa amerudi kugaa-gaa matopeni (2Petro 2:18-22. Maneno mepesi kutilia mkazo)
Kwanza: Ona Petro aliandika kwamba waalimu wa uongo “huwahadaa watu walioanza kuwakimbia wale wanaoenenda katika udanganyifu (2:18). Petro bila shaka alikuwa anawaandikia Wakristo wa kweli, kwa sababu wao walianza kuwakimbia wale wanaoenenda katika udanganyifu, yaani wasioamini. Pia, Petro alisema kwamba wao “walikwisha kuyakimbia machafu ya dunia kwa kumjua Bwana na Mwokozi Yesu Kristo” (2:20). Maana ya pekee ya maneno hayo ni kwamba walikuwa wamezaliwa mara ya pili na hawakuwa wanaendelea kutenda dhambi. (Ona kitu ambacho Petro alikihesabu kuwa alama ya mwamini wa kweli.) Walikuwa hai kiroho.
Lakini Petro anasema, “walinaswa tena” katika kile kilichowachafua zamani, na waka”shindwa” (2:20). Matokeo ni kwamba, “hali yao ya mwisho imekuwa mbaya kuliko ile ya kwanza” (2:20). Kama ni hivyo, bado wangekuwa hai kiroho na wanaokwenda mbinguni? Hapana bila shaka. Petro anawalinganisha na mbwa wanaorudia matapiko yao, na nguruwe wanaorudia matope yao. Je, tufikiri kwamba watu hao kweli wako hai kiroho, na ni watoto wa Mungu, ambao ndani yao Roho Mtakatifu anakaa, na wako kwenye njia hakika ya kwenda mbinguni?
Ushuhuda Wa Yohana
Mtume Yohana bila shaka aliamini kwamba mtu aliye hai kiroho anaweza kufa kiroho. Anasema hivi:
Mtu akimwona ndugu yake anatenda dhambi isiyo ya mauti, ataomba, na Mungu atampa uzima kwa ajili ya hao watendao dhambi isiyo ya mauti. Iko dhambi iliyo ya mauti. Sisemi ya kwamba ataomba kwa ajili ya hiyo. Kila lisilo la haki ni dhambi, na dhambi iko isiyo ya mauti. Twajua ya kuwa kila mtu aliyezaliwa na Mungu hatendi dhambi; bali yeye aliyezaliwa na Mungu hujilinda, wala yule mwovu hamgusi (1Yohana 5:16-18).
Kwanza: Ona kwamba Yohana alikuwa anazungumza juu ya Wakristo kutenda dhambi.
Pili: Ona kwamba Yohana hakuamini kwamba dhambi yoyote au kila dhambi ambayo Mkristo anaweza kutenda inaweza kusababisha kifo chake, kama wengine wenye msimamo mkali. Lakini, Yohana aliamini kwamba ipo “dhambi ya mauti” na kwamba haikuwepo haja ya kuomba kwa ajili ya ndugu aliyetenda dhambi hiyo. Tunaweza kujadili kwa kirefu kwamba dhambi hiyo ni ipi, lakini kwa sasa itatosha tu kusema dhambi hiyo ipo.
Je, Yohana alimaanisha kwamba kuna dhambi isababishayo mauti ya kimwili? Kuna wengi wanaodhani hivyo, hasa kwa sababu mafundisho yao hayatoi nafasi kwa mtu aliye hai kiroho kufa kiroho. Lakini tunapotazama mantiki kabla na baada ya maneno ya Yohana, alikuwa anazungumzia uzima wa milele katika kuandika kwake (ona 1Yohana 5:13, 20). Dhambi ya mauti ni dhambi inayomaliza uzima wa milele.
Yesu Aliwaonya Wafuasi Wake Kuhusu Jehanamu
Hata Yesu aliamini kwamba wokovu wa sasa si uhakikisho kabisa juu ya wokovu ujao. Aliwaonya wanafunzi Wake Mwenyewe wamwogope “yule awezaye kuuangamiza mwili na roho katika jehanamu” (Mathayo 10:28). Hebu fikiri pia maneno Yake kama yalivyoandikwa katika Luka 12:35-46, anayowaambia wanafunzi Wake.
“Viuno vyenu na viwe vimefungwa, na taa zenu ziwe zinawaka; nanyi iweni kama watu wanaomngojea bwana wao atakaporudi kutoka arusini, ili atakapokuja na kubisha, wamfungulie mara. Heri watumwa wale ambao bwana wao ajapo atawakuta wanakesha. Amin nawaambieni, atajifunga na kuwakaribisha chakulani, atakuja na kuwahudumia. Na akija zamu ya pili au akija zamu ya tatu na kuwakuta hivi, heri watumwa hao. Lakini fahamuni neno hili: Kwamba mwenye nyumba angalijua saa atakayokuja mwivi, angalikesha, wala asingaliacha nyumba yake kuvunjwa. Nanyi jiwekeni tayari, kwa kuwa saa msiyodhani ndipo ajapo Mwana wa Adamu.”
“Petro akamwambia, ‘Bwana! Mithali hiyo umetuambia sisi tu, au watu wote pia?’ Bwana akasema, ‘Ni nani basi, aliye wakili mwaminifu mwenye busara, ambaye bwana wake atamweka juu ya utumishi wake wote, awape watu posho kwa wakati wake? Heri mtumwa yule ambaye bwana wake ajapo atamkuta anafanya hivyo. Kweli nawaambia, atamweka juu ya vitu vyake vyote. Lakini mtumwa yule akisema moyoni mwake, ‘Bwana wangu anakawia kuja’, akaanza kuwapiga wajoli wake wanaume kwa wanawake, akila na kunywa na kulewa; bwana wake mtumwa huyo atakuja siku asiyodhani na saa asiyojua, atamkata vipande viwili na kumwekea fungu lake pamoja na wasioamini” (Maneno mepesi kutilia mkazo).
Hata Mathayo aliandika juu ya maonyo hayo ya Yesu, pamoja na mafafanuzi Yake kuhusu hatima ya mwisho ya yule mtumishi asiyekuwa mwaminifu, kwamba “huko kutakuwa na kilio na kusaga meno” (Mathayo 24:51). Basi, kulingana na Yesu, mtu ambaye alikuwa anamtumikia Bwana mwanzoni bado anaweza kupotea kama atarudia maisha ya dhambi.
Ona kwamba yule mtumwa aliyerudi nyuma katika mfano huu ana sifa ya kuwachukia watumwa wenzake na ulevi, dhambi miili ambazo zinaonyesha kwamba mtu hajaokoka (ona 1Yohana 3:13-15; 1Wakor. 6:10).
Ona pia kwamba Yesu alikuwa anazungumza mfano huu kwa wanafunzi Wake mwenyewe, kama inavyotajwa katika Luka 12:22 na 41. Wokovu wa sasa si uhakikisho wa wokovu wa baadaye. Ni lazima tuendelee katika imani hai. Mifano miwili inayofuata katika Injili ya Mathayo – ule wa Wanawali Kumi na Talanta – pia hutusaidia kuona ukweli wa jambo hilo (ona Mathayo 25:1-30).
Hoja ya Yesu ni dhahiri mno kiasi cha kwamba wale wanaoamini fundisho la uongo kuhusu usalama wa milele wa wokovu bila kujali chochote wanalazimika kusema kwamba “giza la nje” ambako kutakuwepo na “kilio na kusaga meno” ni mahali fulani huko mbinguni ambapo Wakristo wasiokuwa waaminifu sana watakwenda ili kuomboleza kwa muda juu ya kupoteza kwao thawabu zao!
Yesu pia alilionya kanisa la Sardi juu ya hatari ya waamini waliozaliwa mara ya pili kufa kiroho. Inaonekana kwamba wengi katika Wakristo wa Sardi walikuwa wamerudia dhambi. Basi walikuwa katika hatari ya kutovikwa mavazi meupe, na kwamba Yesu asingewakiri mbele za Baba Yake, na majina yao yangefutwa kutoka katika kitabu cha uzima. Lakini bado walikuwa na muda wa kutubu. Hebu jisomee vizuri na polepole anachosema.
Nayajua matendo yako, ya kuwa una jina la kuwa hai nawe umekufa. Uwe mwenye kukesha, ukayaimarishe mambo yaliyosalia, yanayotaka kufa. Maana sikuona matendo yako kuwa yametimilika mbele za Mungu wangu. Basi kumbuka jinsi ulivyopokea, na jinsi ulivyosikia; yashike hayo na kutubu. Walakini usipokesha, nitakuja kama mwivi, wala hutaijua saa nitakayokuja kwako. Lakini unayo majina machache katika Sardi, watu wasioyatia mavazi yao uchafu. Hao watakwenda pamoja nami hali wamevaa mavazi meupe, kwa kuwa wamestahili. Yeye ashindaye atavikwa hivyo mavazi meupe, wala sitalifuta kamwe jina lake katika kitabu cha uzima, nami nitalikiri jina lake mbele za Baba yangu, na mbele za malaika zake” (Ufunuo 3:1-5. Maneno mepesi kutilia mkazo.)
Pamoja na hayo ambayo Yesu, na Petro, na Yakobo, na Yohana na Paulo walifundisha, inakuwaje kwamba waalimu wengi wa siku hizi wanadai kwamba kama mtu ameokoka kweli hawezi kupoteza wokovu wake hata kama anaishi maisha gani? Huo ni ongo kutoka kwa Shetani kabisa, ulioanza wakati alipomwambia mtu hai kiroho aliyekuwa anafikiri kutenda dhambi, kwamba “Hakika hamtakufa!” (Mwanzo 3:4). Mbona Wakristo wengi wasitambue huo uongo wa tangu mwanzo wa Shetani, ambao unaenezwa na mafundisho ya kisasa ya uongo?
Wakati Mwamini Anapoacha Kuamini
Kutokuwa mwenye haki si hatari ya pekee kwa waaminio. Kama mwamini wa kweli ataacha kuamini, atapoteza wokovu wake maana wokovu umeahidiwa kwa wale tu wanaoamini na wanaoendelea kuamini. Agano Jipya la Kiyunani linapozungumza kuhusu wokovu, linatumia neno kuamini katika hali ya kuendelea. Wokovu ni kwa wale wanaoamini na wanaoendelea kuamini, si kwa wale walioamini wakati fulani zamani. Kwa sababu hiyo na nyingine, Agano Jipya limejaa mashauri yenye kuwaonya waamini waendelee kwenye njia ya haki. Yesu aliwaonya wanafunzi Wake Mwenyewe kwamba “atakayevumia mpaka mwisho, huyo ndiye atakayeokoka” (Mathayo 10:22).
Ona maneno ya Paulo kwa Wakristo Wakolosai juu ya jambo hili.
Na ninyi, mliokuwa hapo kwanza mmefarakanishwa, tena adui katika nia zenu kwa matendo yenu mabaya, amewapatanisha sasa katika mwili wa nyama yake, kwa kufa kwake, ili awalete ninyi mbele zake, watakatifu, wasio na mawaa wala lawama; mkidumu tu katika ile imani, hali mmewekwa juu ya msingi, mkawa imara; msipogeuzwa na kuliacha tumaini la Injili mliyosikia habari zake, iliyohubiriwa katika viumbe vyote vilivyo chini ya mbingu (Wakolosai 1:21-23. Maneno mepesi ni kutilia mkazo.)
Wengi wanaofuata mafundisho ya Calvin wanadai maana ya Paulo ni kwamba, Wakristo wote wa kweli wataendelea kudumu katika imani mpaka kifo, na kama wakati fulani wataacha kuamini, hiyo inathibitisha kwamba hawakuwahi kuokoka wakati wowote. Kwa sababu ya waamini wengi wanaozaa matunda ambao huanguka, baadhi ya wanaCalvin pia hudai kwamba Mkristo wa bandia, ambaye hajajazwa na Roho Mtakatifu anaweza kuonekana kama mwamini wa kweli. Anaweza hata kuonyesha matunda zaidi ya Roho kuliko Wakristo wa kweli, lakini mwishowe atakwenda jehanamu kwa saabu hakuwa na imani ya wokovu! Sasa ni kwamba mwanaCalvin ambaye lazima asimamie mafundisho yake inambidi kila wakati aishi huku kukiwa na uwezekano kwamba imani yake inaweza kuthibitishwa kuwa ya bandia kama ataacha kuamini. Ikiwa imani halisi ya kipekee ni ile imani inayovumilia mpaka kifo, basi mwanaCalvin hawezi kuwa na uhakika wa wokovu wake, maana hatajua kama imani yake ni halisi mpaka anapovuta pumzi yake ya mwisho. Hapo ndipo atakapojua kama imani yake ilidumu hadi kifo na kuthibitisha kwamba ilikuwa ya kweli.
Nadharia hiyo ni kinume na mawazo ya Paulo katika Wakolosai 1:23. Yeye aliwataka Wakristo Wakolosai wajue kwamba wakati huu walikuwa wamepatanishwa na Mungu, na kwamba wangeendelea kuwa na msimamo huo huo bila hatia mbele Zake, kama wangedumu kuamini.
Angalia pia maneno ya Paulo kuhusu wokovu wa Wakorintho.
Basi ndugu zangu, nawaarifu ile injili niliyowahubiri; ambayo ndiyo mliyoipokea, na katika hiyo mnasimama, na kwa hiyo mnaokolewa ikiwa mnayashika sana maneno niliyowahubiri … (1Wakor. 15:1, 2 – Maneno mepesi kutilia mkazo).
Paulo aliwahakikishia wokovu wao, kutokana na imani yao. Wangedumu kuwa wameokoka kama wangeshikilia Injili. Hakuwaambia wakati huo kwamba kitakachoamua ni muda, kama kweli wameokoka, ikiwa watadumu katika imani mpaka kufa.
Linda Moyo Wako Na Kutokuamini
Mwandishi wa kitabu cha Waebrania alionya kuhusu hatari za kweli za kuruhusu kutokuamini au dhambi kuingia maishani mwetu. Ona kwamba anawaambia ndugu Wakristo maneno haya yafuatayo:
Angalieni ndugu zangu, usiwe katika mmoja wenu moyo mbovu wa kutokuamini, kwa kujitenga na Mungu aliye hai. Lakini mwonyane kila siku maadamu iitwapo leo; ili mmoja wenu asifanywe mgumu kwa udanganyifu wa dhambi. Kwa maana tumekuwa washirika wa Kristo, kama tukishikamana na mwanzo wa uthabiti wetu kwa nguvu mpaka mwisho (Waebrania 3:12-14. Maneno mepesi kutilia mkazo).
Sisi ni “washirika wa Kristo” muda wote tutakao”shikamana” katika imani. Dhambi ina uwezo wa kutudanganya na kutufanya wagumu, basi, tujihadhari na kutokuamini pamoja na dhambi, visiingie maishani mwetu.
Baadaye katika barua yake, mwandishi wa kitabu cha Waebrania anataja maneno ya maandiko maarufu sana katika Agano la Kale – Habakuki 2:4 – kisha, anaongezea yafuatayo, chini ya uvuvio:
‘Lakini mwenye haki wangu ataishi kwa imani; Naye akisitasita, roho yangu haina furaha naye.’ Lakini sisi hatumo miongoni mwao wasitao na kupotea, bali tumo miongoni mwa hao walio na imani ya kutuokoa roho zetu (Waebrania 10:38-39. Maneno mepesi kutilia mkazo.)
Je, kuna kuwa wazi kuliko hivyo?
Kupandikizwa Na Kuvunjwa
Miongoni mwa maandiko mengine mengi, Warumi 11:13 hadi 24 pia husimama kama ushahidi kwamba waamini wa kweli wanaweza kupoteza wokovu wao kama wataacha imani yao. Hili ni jambo ambalo kila msomaji aliye mkweli atakubali. Angalia yafuatayo:
Lakini nasema na ninyi mlio watu wa Mataifa. Basi, kwa kadiri nilivyo mtume wa watu wa Mataifa, naitukuza huduma iliyo yangu, nipate kuwatia wivu walio damu moja na mimi na kuwaokoa baadhi yao. Maana ikiwa kutupwa kwao kumeleta upatanisho kwa ulimwengu, je! Kukubaliwa kwao kutakuwa nini kama si uhai baada ya kufa? Tena malimbuko yakiwa matakatifu, kadhalika na donge lote; na shina likiwa takatifu, matawi nayo kadhalika. Lakini iwapo matawi mengine yamekatwa na wewe mzeituni mwitu ulipandikizwa kati yao, ukawa mshirika wa shina la mzeituni na unono wake, usijisifu juu ya matawi yale; au ikiwa wajisifu, si wewe ulichukuaye shina, bali ni shina likuchukualo wewe. Basi utasema, ‘Matawi yale yalikatwa kusudi ili nipandikizwe mimi.’ Vema, yalikatwa kwa kutokuamini kwao, na wewe wasimama kwa imani yako. Usijivune, bali uogope. Kwa maana ikiwa Mungu hakuyaachia matawi ya asili, wala hatakuachia wewe. Tazama basi, wema na ukali wa Mungu. Kwa wale walioanguka, ukali, bali kwako wewe wema wa Mungu, ukikaa katika wema huo; kama sivyo, wewe nawe utakatiliwa mbali. Na hao pia, wasipokaa katika kutokuamini kwao, watapandikizwa; kwa kuwa Mungu aweza kuwapandikiza tena. Kwa maana ikiwa wewe ulikatwa ukatolewa katika mzeituni, ulio mzeitumi mwitu kwa asili yake, kisha ukapandikizwa kinyume cha asili katika mzeituni ulio mwema, si zaidi sana wale walio wa asili kuweza kupandikizwa katika mzeituni wao wenyewe? (Warumi 11:13-24. Maneno mepesi kutilia mkazo.)
Basi, ni dhahiri kwamba upo uwezekano wa kupoteza nafasi yako kwenye mti wa Mungu wa wokovu. Tunasimama kwa imani yetu na tunahakikishwa nafasi yetu tukikaa “katika wema Wake” tu (11:22).
Turudie Tena Adhabu Ya Mungu
Baada ya hayo yote, hebu turudi tena kwenye maneno ya Paulo kuhusu adhabu ya Mungu katika 1Wakorintho 11:27 hadi 34, na tuulize swali lingine: Je, adhabu ya Mungu inahakikisha kwamba Mkristo mwenye dhambi atatubu na kutokuhukumiwa kama dunia?
Jibu bila shaka ni hapana kwa sababu kadha. Kwanza ni kwa sababu ya maandiko yale yote ambayo tumesoma, yenye kuonyesha kwamba mwamini wa kweli anaweza kupoteza wokovu wake kwa kuacha imani yake au kurudia matendo yasiyo haki. Mwamini yeyote anayepotea bila shaka anapendwa na Mungu, na Maandiko yanafundisha kwamba Yeye humwadhibu kila ampendaye (Waerania 12:6). Lakini, kwa kuwa inawezekana kwa waamini kurudi kwenye kutokutenda haki au kutokuamini na hatimaye kufa kiroho, tunachoweza kusema tu ni kwamba adhabu ya Mungu haiwarudishi kila mara wale wanaopotea.
Pili: Mungu kamwe haweki pembeni hiari yetu kwa habari ya wokovu wetu. Kama hatutaki kumtumikia, hakuna lazima, na Biblia inatoa mifano ya watu wengi sana ambao Mungu aliwaadhibu na hawakutubu. Kwa mfano: Mfalme Asa alikuwa mfalme mzuri sana mwanzoni. Lakini baadaye maishani mwake alifanya dhambi na akakataa kutubu hata wakati akipata adhabu ya Mungu ambayo ilikuwa maradhi katika miguu yake. Mwishoni, ugonjwa huo ulimwua (ona 2Nyakati sura ya 14 hadi 16).
Kulingana na mwandishi wa kitabu cha Waebrania, inawezekana kabisa kwa watoto wa Mungu kuitikia vibaya adhabu ya Mungu. Anasema hivi juu ya hilo:
Tena mmeyasahau yale maonyo yasemayo nanyi kama kusema na wana, ‘Mwanangu, usiyadharau marudia ya Bwana, wala usizimie moyo ukikemewa naye…’ Na pamoja na hayo tulikuwa na baba zetu wa mwili walioturudi, nasi tukawastahi; basi si afadhali sana kujitia chini ya Baba wa roho zetu na kuishi? (Webrania 12:5, 9).
Wakati tunapoadhibiwa na Baba yetu, tunaweza “kudharau” au “kunywea”, yaani, tunaweza kushindwa au kulemewa na kuachia mbali. Lakini Mungu anatamani kwamba tujinyenyekeze na kukubali adhabu Yake ili “tuishi”. Ni dhahiri kwamba kama tutakataa kujinyenyekeza hatutaishi, tutakufa. Mwandishi bila shaka alikuwa anaandika kuhusu maisha ya kiroho (na bila shaka kifo cha kiroho), kwa sababu hata Wakristo watii hatimaye hufa kimwili, licha ya ukweli kwamba wengi ambao hawako chini ya “Baba wa roho zetu” huendelea kuishi kimwili kwa muda mrefu sana.
Hili linatufikisha kwenye swali linalofuata: Vipi kuhusu kifo cha kimwili kabla ya wakati wake? Kama ni aina moja ya adhabu ya Mungu, ambayo kusudi lake ni kwamba “tusihukumiwe pamoja na dunia”, si ingekuwa vizuri kwa Bwana kumpeleka nyumbani kila Mkristo atendaye dhambi, kabla ya kufa kiroho?
Kama mambo yangekuwa hivyo kila wakati, isingewezekana kwa mtu kupoteza wokovu wake. Kama mtu ameokoka, asingekuwa na haja ya kuwa na wasiwasi juu ya kuacha imani yake au kurudia tabia ya dhambi, maana angetulia kwa uhakika kwamba Bwana atafupisha maisha yake kabla ya kufa kiroho na kupoteza wokovu wake. Lakini, wazo hili linapingana na maandiko mengi yenye kuonyesha kwamba kweli mtu aliyeokoka anaweza kupoteza wokovu wake. Sasa, jibu ni nini?
Labda mfano wa kibinadamu unaweza kutusaidia – Mwananchi anaweza kuvunja sheria na kupata adhabu ya serikali. Lakini, akikimbia nchi atakuwa amejiondoa kwenye mamlaka ya serikali hiyo. Basi, hatapatikana na adhabu ya serikali wala hawezi kushiriki faida za wananchi.
Au mfano mwingine: Mtoto anaweza kukataa kumtii baba yake na kupata adhabu yake ya upendo. Lakini kama mtoto huyo atatoroka nyumbani na kwenda kufanya kile ambacho baba yake anakataa, hana haja ya kuhofu adhabu ya baba yake. Amekwisha kujiondoa kwenye familia ile. Basi, kwa wale wanaoiacha imani yao au wanaorudi moja kwa moja kwenye kuufuata mwili, faraja ya adhabu iliyoahidiwa, na ikibidi, kifo kabla ya wakati, si vitu vinavyowezekana. Wanakuwa wamepoteza kila kitu kilichokuwa chao. Wanaweza kufa kabla ya wakati kweli, lakini hawaendi mbinguni hatimaye.
Lakini, wale miongoni mwa watoto wa Mungu wanaojikwaa na kuingia katika dhambi, lakini ambao mioyo bado inataka kumtumikia Mungu, wanajiweka katika nafasi ya kuadhibiwa na Baba yao kama hawajihukumu wenyewe kwa toba na kuungama. Hawa watoto kwa kawaida ni watii: hawakimbii wala kuitoroka familia yao, ila, kwa kiwango fulani si watiifu. Kama wataendelea katika kutokutii kwao, wakiacha kuungama na kutubu dhambi zao, wanaweza kuhukumiwa kwa kifo cha kimwili kabla ya wakati, ila wanapokufa bado wameokoka.
Kwa mfano: Mungu anaweza kumwita mtoto Wake mmoja awe mchungaji. Kama huyo mtoto wa Mungu atapingana na mwito huo, anaweza kupatikana na adhabu ya Mungu kwa namna fulani. Akidumu katika kutokutii anaweza kufa kabla ya wakati, lakini bado atakwenda mbinguni. Si kwamba aliishi “kwa kuufuata mwili,” bali alikuwa anayafisha matendo ya mwili kwa Roho. Alikuwa na matunda maishani mwake, lakini alikuwa anapungua kwenye kile ambacho Mungu alitazamia. Yeye si kama Mkristo ambaye ameacha imani yake au kurudia matendo ya dhambi.
Tunaweza kujiuliza hivi: “Ni kitu gani ambacho ni kibaya kuhusu kufa kabla ya wakati, na kwenda mbinguni? Si hiyo ni thawabu nzuri zaidi kuliko adhabu?”
Swali kama hilo linafunua kutokuelewa kwetu jinsi ambavyo Mungu atawapa thawabu kubwa wale watauwa katika maisha yajayo. Ikiwa hata kutoa kikombe cha maji baridi tu kutasababisha thawabu; ikiwa kwa kuvumilia “dhiki ndogo ya muda” tutazamie “utukufu wa uzito upitao” (2Wakor. 4:17); ikiwa kwa kuwapa wenye mahitaji tunaweza kujiwekea “hazina mbinguni” (Luka 12:33), basi kila sekunde tunayoweza kumtumikia Mungu hapa duniani inapaswa kuhesabiwa kama nafasi ya hali ya juu sana. Ni huzuni sana tunapopoteza wakati ambao hatuwezi kuupata tena. Katika siku zijazo, tutatazama nyuma kwa majuto makubwa sana. Hii itakuwa kweli sana kwa wale waliokufa kabla ya wakati na hawakupata nafasi zaidi za kumtumikia Bwana hapa duniani.
Je, Magonjwa Yote Ni Ishara Ya Adhabu Ya Mungu?
Ni dhahiri kutokana na yale ambayo Paulo aliwaandikia Wakorintho, udhaifu, magonjwa na kifo kabla ya wakati vinaweza kuwa madhihirisho ya adhabu ya Mungu. Ingawa haitakuwa sawa kufikia mahali pa kusema kwamba udhaifu wote, magonjwa au kifo kabla ya wakati ni onyesho la adhabu ya Mungu, yapo Maandiko mengine mengi licha ya 1Wakorintho 11:27-32 yenye kushuhudia uwezekano huo. Hivyo basi, Mkristo yeyote anayejikuta akiteseka kimwili atakuwa na busara kutafuta muda wa kujichunguza. Ikiwa tunapitia katika adhabu ya Mungu, inaonekana haiwezekani kwamba tupate nafuu ya kudumu kimwili bila ya toba na msamaha wa Mungu.
Adhabu ya Mungu kweli inaweza kuja kwa njia nyingine zaidi ya ugonjwa wa kimwili. Mungu anaweza kupanga mazingira kwa njia mbalimbali ili kukamilisha makusudi Yake. Yakobo ambaye wakati mmoja alijifanya ni ndugu yake ili kumdanganya baba yake, aliamka asubuhi fulani akiwa ameoa mwanamke ambaye alijifanya ndiye mpenzi wake! Wakristo wengi ambao si watii wamewahi kuamkia katika mazingira kama hayo, wakati Bwana alipowafundisha polepole juu ya kupanda na kuvuna.
Zaidi ya yote, tusisahau kwamba adhabu ya Mungu ni ishara ya pendo Lake kwetu. Mkristo anayepata adhabu asifikiri jambo lingine lolote. Yesu alisema hivi: “Wote niwapendao mimi, ninawakemea na kuwarudi; basi uwe na bidii, ukatubu” (Ufunuo 3:19 – Maneno mepesi kutilia mkazo). Mwandishi wa kitabu cha Waebrania anatwambia kwamba Mungu hushughulika nasi kama baba yeyote mwema anavyofanya na mtoto wake:
Maana mtafakarini sana yeye aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao dhambi juu ya nafsi zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu. Hamjafanya vita hata kumwagika damu, mkishindana na dhambi; tena mmeyasahau yale maonyo yasemayo nanyi kama kusema na wana:
“Mwanangu, usiyadharau marudia ya Bwana,
wala usizimie moyo ukikemewa naye;
Maana yeye ambaye Bwana ampenda humrudi,
Naye humpiga kila mwana amkubaliye.”
Ni kwa ajili ya kurudiwa mwastahimili; Mungu awatendea kama wana; maana ni mwana yupi asiyerudiwa na babaye? Basi kama mkiwa hamna kurudiwa, ambako ni fungu la wote, ndipo mmekuwa wana wa haramu ninyi, wala si wana wa halali. Na pamoja na hayo tulikuwa na baba zetu wa mwili walioturudi, nasi tukawastahi; basi si afadhali sana kujitia chini ya Baba wa roho zetu na kuishi? Maana ni hakika hao kwa siku chache waliturudi kama walivyoona vema wenyewe; bali yeye kwa faida yetu, ili tuushiriki utakatifu wake. Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani (Waebrania 12:3-11).
Ukifikiri vizuri juu ya kile tulichosoma sasa hivi, inaonekana kwamba tunapaswa kujali ikiwa hatuadhibiwi kuliko kama tunaadhibiwa! Mwandishi wa Waebrania aliandika kwamba “wote tumekuwa washirika” wa adhabu ya Mungu, na wale ambao hawahusiki ni “wana wa haramu, si wana wa halali” (12:8).
Mungu anatamani kwamba tushiriki utakatifu Wake. Hilo ndilo kusudi Lake tangu mwanzo. Kuadhibiwa si kitu kizuri, lakini baada ya kuvumilia na kupitia, huleta haki maishani mwetu. Mtunga Zaburi aliandika hivi: “Kabla sijateswa mimi nalipotea, lakini sasa nimelitii neno lako … Ilikuwa vema kwangu kuwa naliteswa, nipate kujifunza amri zako” (Zaburi 119:67; 71).
Wakati Kanisa Linapotekeleza Adhabu Ya Mungu
Kuna sehemu moja nyingine ya adhabu ya Mungu ambayo tunahitaji kuiangalia. Hiyo nayo ni kitu ambacho Mungu hutumia kutuhamasisha kuwa watakatifu. Ni adhabu inayotolewa na kanisa.
Kwa bahati mbaya sana, maneno ya Yesu juu ya jambo hilo hayatiliwi maanani sana. Kimsingi ni kwa sababu mara nyingi mtazamo wa makanisa mengi na wengi wanaojiita Wakristo si utakatifu wa kibinafsi wala wa kusanyiko. Lakini, Wakristo wa kweli ambao wanajitahidi pamoja kumpendeza Bwana hawatapuuza maneno ya Yesu aliyosema, hivi:
“Na ndugu yako akikukosa, enenda ukamwonye wewe na yeye peke yenu; akikusikia, umempata nduguyo. La kama hasikii, chukua pamoja nawe tena mtu mmoja au wawili, ili kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila neno lithibitike. Na asipowasikiliza wao, liambie kanisa; na asipolisikiliza kanisa pia, na awe kwako kama mtu wa mataifa na mtoza ushuru” (Mathayo 18:15-17).
Mtu haachi kushangaa kitu kinachoweza kutokea ikiwa amri hizo zitatiliwa mkazo kanisani. Bila shaka katika makanisa mengi mahudhurio yangepungua. Ni wazi kwamba kama washirika wa mwili wa Kristo tunao wajibu, si kwa ajili ya utakatifu wetu tu, bali pia tunawajibika kiasi fulani kwa ajili ya utakatifu wa waamini wengine na usafi wa kanisa la Kristo.
Ni vizuri kufikiri kwamba maneno ya Yesu kuhusu adhabu ya kanisa yanahusu zile nyakati ambazo ndugu hutukosea kibinafsi, na si wakati ndugu anapotenda dhambi kwa ujumla. Hii tafsiri inatiwa nguvu kwa maneno ya Yesu yaliyoandikwa katika Luka 17:3-4: “Jilindeni; kama ndugu yako akikukosa, mwonye; akitubu msamehe. Na kama akikukosa mara saba katika siku moja na kurudi kwako mara saba, akisema ‘Nimetubu’ msamehe” (maneno mepesi kutilia mkazo). Ona Yesu alivyosema: “Kama akikukosea.” Pia, Yesu alitwambia tumsamehe ndugu yeyote anayetubu na ambaye tunamkemea. Tunaweza kusamehe makosa ya binafsi ya wengine, lakini si dhambi zao za jumla. Tena, tunaona kwamba baada ya kufuata maneno ya Yesu kuhusu adhabu ya kanisa katika Mathayo 18 ni mfano wa mtumishi asiyesamehe, uliotokana na swali la Petro kwamba ni mara ngapi amsamehe ndugu yake. Katika swali la Petro na jibu la Yesu katika mfano huo kuna wazo la makosa ya kibinafsi.
Utaratibu Wenyewe
“Adhabu ya kanisa” haipaswi kuhusisha kusanyiko lote, isipokuwa mara chache sana. Huanza na mtu mmoja ambaye amejitoa kuwa mtakatifu. Lazima ni mtakatifu kwa sababu kama mbili hivi. Kwanza: Kama yeye si mtakatifu kibinafsi kwa kiwango fulani, atakuwa na sehemu ile ya mtu mwenye boriti katika jicho lake, anayejaribu kutoa kibanzi katika jicho la mwingine (ona Mathayo 7:3-5). Je, nina haki gani ya kumrekebisha ndugu anayetenda dhambi, kama mimi ni mwenye dhambi zaidi?
Pili: Kama kosa lililotendwa ni la kibinafsi, basi huyo aliyekosewa lazima awe mtakatifu kiasi cha kutosha kuhitaji mapatano. Wengi wetu tunapokosewa, tunazungumza na kila mtu juu ya kukosewa huko isipokuwa yule mkosaji. Tunapenda kusengenya badala ya kutafuta mapatano. Maandiko yanatuonya kwamba tunapofanya hivyo, tuko katika hatari ya hukumu (ona Mathayo 7:1-2; Yakobo 4:11; 5:9).
Basi – Hebu tufikiri kwamba mwamini ametenda dhambi, na tuseme amekukosea. Unachotakiwa ni kumwendea na kusema naye kwa upendo, upole na unyenyekevu. Mara nyingi utagundua kwamba yule mkosaji hakutambua alichofanya, na atakuomba msamaha mara moja. Wewe unachotakiwa kufanya ni kumsamehe, na unaweza kutaka kuhoji maswali kama ni mtu mwenye kuumia sana. Mara nyingi, “makosa” ambayo watu “yanawaumiza” yanatakiwa kupuuzwa kwa kudhani kwamba mhusika hakukusudia madhara. Kwa mfano: Kwa kuwa ilionekana kana kwamba mchungaji wako alikuwa anakukwepa kanisani haimaanishi kwamba alikuwa anakukwepa. Pengine alikuwa akishughulika na kuwatafuta wengine.
Uwezekano mwingine unapomkabili yule ndugu ni kwamba anaweza kukujulisha mchango wako na wewe katika kosa lile. Pengine anaweza kukwambia kwamba alifanya hicho alichofanya kwa sababu wewe ulimkwaza. Kama ni hivyo, alitakiwa kuwa ameshakuja kwako. Lakini, sasa unatambua kwamba wewe ndiye uliyesababisha tatizo, na unahitaji kuomba msamaha. Hapo ndugu yako atawajibika kukusamehe, na mapatano yatakuwepo.
Hatua Ya Pili Na Ya Tatu
Hebu tuseme kwamba hakuna lolote katika hayo hapo juu kinachotokea. Yule mkosaji anakataa kukubali kosa lake au kukuomba msamaha. Hapo sasa, “chukua mwingine mmoja au wawili umwendee, ili kwa kinywa cha mashahidi wawili au watatu kila jambo lithibitishwe” (Mathayo 18:16).
Ni hivi: Kabla ya kuwashawishi hao wengine wamkabili mkosaji, itakubidi uwashawishi juu ya jambo unalotaka kufanya. Wanaweza kutaka kumhoji mkosaji kabla ya kukubaliana nawe. Wanaweza hata kushawishika kwamba mkosaji anayedaiwa si mkosaji, wakakurekebisha wewe! Kama ni hivyo, wewe unapaswa kumwomba msamaha “yule mkosaji”!
Ila, ukiweza kuwashawishi wengine kwamba wewe ndiye mwenye haki katika jambo hilo, basi kwa pamoja mnakwenda kumkabili yule mkosaji tena. Inatazamiwa kwamba wao kuungana na wewe kutatosha kumfanya yeye akiri kosa lake na kuomba msamaha, jambo ambalo litaleta mapatano.
Lakini tena, kama bado anakataa kukiri kosa lake – japo haitokei mara nyingi – basi jambo hilo lifikishwe mbele ya kanisa zima. Maana yake ni kwamba uongozi wa kanisa utahusishwa. Bila shaka watataka kuchunguza kila kitu kikamilifu kabla ya kuamua kujiunga na wewe. Hapo tena kuna uwezekano kwamba wanaweza kugundua kwamba wote wawili mna madai halali, na kwamba wote wawili mnahitaji kuombana msamaha. Lakini, wakikuunga mkono ujue kwamba una madai halali dhidi ya ndugu yako.
Akigundua kwamba kanisa zima limeungana na wewe na linapanga kumkabili, aidha atatubu au ataondoka kanisani. Hakutakuwa na haja ya kumtenga. Yesu alisema awe kama “mtu wa Mataifa na mtoza ushuru” (18:17). Yaani, ahesabiwe kama mtu ambaye hajaokoka, kwa sababu inaonekana ndivyo alivyo. Mtu ambaye amezaliwa mara ya pili hawezi kupingana na uamuzi wa kanisa zima. Basi, ahesabiwe kwamba si mwamini – ni mtu anayehitaji kushuhudiwa tena na kuzaliwa mara ya pili.
Kama Mkosaji Atatubu …
Ikiwa wakati wowote kabla au wakati mambo yanaendelea kushughulikiwa au baada ya adhabu hiyo ya kanisa kutolewa, mhusika ataomba msamaha, lazima asamehewe la sivyo ninyi mtapata adhabu ya Mungu. Mara tu baada ya kutoa maelezo juu ya adhabu ya kanisa, Yesu alisimulia kisa juu ya mtumwa aliyekuwa amesamehewa deni kubwa sana na mfalme. Lakini huyo naye akakataa kumsamehe mtumwa mwenzake ambaye alikuwa anamdai kiasi kidogo sana. Akaagiza atupwe gerezani. Mfalme aliposikia juu ya kutosamehe kwa mtumwa wake, “alighadhabika sana” na “akampeleka kwa watesaji, hata atakapoilipa deni ile yote” (Mathayo 18:34). Kisha Yesu akatoa ahadi hii: “Ndivyo na Baba yangu wa mbinguni atakavyowatenda ninyi, msiposamehe kwa mioyo yenu kila mtu ndugu yake” (Mathayo 18:35).
Wengine wanatafsiri onyo la Yesu kwamba ni kupoteza nafasi yetu kama watu waliosamehewa, na kutupwa jehanamu. Ni dhahiri kwamba yule mtumwa ambaye hakusamehe aliwajibishwa juu ya deni lake la zamani, ambalo asingeweza kulilipa, na akajikuta amerudia hali ile aliyokuwa nayo kwanza: kutosamehewa. Je, hii inaonyesha “alipoteza wokovu wake?”
Kuna watakaosema kwamba hiyo ni kuingiza mengi katika maneno ya Yesu kuliko alivyosema. Wangependa kufikiri kwamba Yeye alimaanisha adhabu fulani ya kidunia, na kwamba kule “kupelekwa kwa watesaji” ni kusumbuliwa kidogo na mapepo. Baada ya kuteseka kidogo, atatubu na kumsamehe ndugu yake.
Lakini Yesu aliahidi kwamba tusiposamehe dhambi za wengine, sisi wenyewe hatutasamehewa (ona Mathayo 6:14-15). Je, alimaanisha tutapoteza hali yetu kwamba tumesamehewa, au alimaanisha tu kwamba hatutasamehewa dhambi zozote za baadaye, na kwa njia hiyo kupoteza ushirika na Mungu na baraka fulani za kidunia lakini bado tumeokoka? Paulo alitushauri tusameheane sisi kwa sisi kama ambavyo tumesamehewa pia, lakini hakuongezea kitisho (ona Waefeso 4:32). Mimi nadhani kama Yesu alimaanisha kwamba tunapokataa kumsamehe mwamini mwingine tunaweza kupoteza wokovu wetu, Paulo angetilia mkazo jambo hilo. Lakini tena, ingawa Paulo hakutaja kutokusamehe kuwa ni dhambi ambayo ingesababisha kupotea kwetu kabisa, alisema kwamba mtu akiwa na tabia za dhambi kama vile uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka na husuda hataurithi ufalme wa Mungu (Wagalatia 5:20-21).
Hata kama hatujui tafsiri sahihi ya maneno ya Yesu kuhusu msamaha, mimi siwezi kucheza na wokovu wangu kwa kukataa kumsamehe ndugu aliyetubu. Ni afadhali kusamehe.
Msamaha Bandia
Je, tuna wajibu wa kuwasamehe wale wanaotukosea ambao hawakiri makosa yao? Je, tuwahesabu wakosaji wasiotubu kana kwamba hakuna chochote kilichotokea? Haya ni maswali muhimu yanayowasumbua Wakristo wengi.
Kwanza: Ni lazima tutambue kwamba haiwezekani kuwepo na mapatano ya kweli bila ya kuwasiliana, toba na kusameheana. Hili linaeleweka kirahisi katika ndoa. Mwenzi mmoja anapomkosea yule mwingine, kunakuwa na kutokuelewana. Pengine hata hawazungumzi tena. Mmoja analala kwenye kiti.
Ni kitu gani kitakachorudisha mahusiano yao? Ni mawasiliano, toba na kusameheana. Wanaweza kujaribu kupuuza yaliyotokea. Wanaweza kujilazimisha kuchekeana na kuzungumzia mambo mengine. Lakini bado kuna kitu kati yao. Mahusiano yao yameharibika, na yatabaki hivyo mpaka kuwepo mawasiliano, toba na kusameheana.
Kama mmoja ndiye mkosaji, yule aliyekosewa anaweza kujaribu “kusamehe” huku akijaribu kusahau yaliyotokea na kuendelea na maisha kana kwamba hakuna kilichotokea. Lakini kila anapomwona mkosaji lile kosa linarudi akilini. Anawaza kwa masikitiko, “Mbona siwezi kusamehe?”
Sababu ni kwamba anajaribu kufanya kisichowezekana: Kitu ambacho hata Mungu hafanyi. Mungu huwasamehe wale wanaotubu tu. Hatazamii mwamini aliyekosewa kujifanya kana kwamba hakuna kosa lililotendwa, huku akijaribu kujishawishi kwamba kwa kweli yule aliyemkosea ni ndugu mzuri tu ambaye hana matatizo. Hii ndiyo sababu Yesu alituambia tumkabili mkosaji, na kama hatatubu tumpitishe katika zile hatua za adhabu kikanisa. Lakini, wakati wowote katika hizo hatua, akitubu, hatuna budi kumsamehe. Kama Yesu alitazamia mwamini aliyekosewa “kusamehe” tu na kuendelea na maisha, asingesema alichosema juu ya adhabu kikanisa. Anasema tena kama ifuatavyo:
“Jilindeni! Kama ndugu yako akikosa, mwonye; akitubu, msamehe. Na kama akikukosa mara saba katika siku moja na kurudi kwako mara saba akisema, ‘Nimetubu,’ msamehe” (Luka 17:3, 4 – Maneno mepesi kwa ajili ya kutilia mkazo).
Inawezekana, na ni sawa kutazamia kwamba waamini wote watampenda kila mmoja – hata wakosaji wasiotubu – kama Mungu. Lakini kuwapenda hakumaanishi msamaha bila masharti. Mungu anampenda kila mmoja, lakini si kila mmoja aliyesamehewa Naye.
Yasiyowezekana
Lakini, vipi kama haiwezekani kwa sababu zilizo nje ya uwezo wako, kufuata ule utaratibu wa adhabu kikanisa ambao Yesu aliutoa? Kwa mfano: Umekosewa sana na mwamini ‘maarufu’ kama mchungaji, naye anakataa kuonana na wewe. Au unamkabili mkosaji anayekataa kutubu, na umekosa mtu aliye tayari kurudi kwake na wewe kwa ajili ya hatua ya pili.
Katika hali kama hiyo, maneno ya Paulo yanafaa. Anasema hivi: “Ikiwezekana, kwa upande wenu, kaeni kwa amani na watu wote” (Warumi 12:18, TLR). Fanya unachoweza – hicho ndicho Mungu anachotazamia kwako.
Vyovyote inavyokuwa, kila mara Bwana anataka sisi tugeuze “shavu la pili” na kwenda “maili ya pili”. Kama nilivyokwisha kusema mwanzoni, hii haimaanishi turuhusu kuonewa au kutendewa mabaya. Maana yake ni kwamba tufanye zaidi ya matazamio ya watu. Hiyo ni kweli hasa tunaposhughulika na wasioamini. Wao hawajadai kwamba ni wafuasi wa Kristo. Kwa hiyo, kujaribu kuwapitisha kwenye ule utaratibu ambao Mungu amekwisha utoa kwa kanisa ni upuzi.
Kama nilivyokwisha sema, ingawa Mungu hamsamehe mtu mpaka atubu, bado anawapenda watu wasiotubu na anawasubiri kwa upendo na mikono wazi kuwapokea wakati wowote. Hiyo ndiyo inayotakiwa kuwa hali yetu ya moyo kwa habari ya mkosaji yeyote asiyetubu. Hatuwezi kumsamehe mpaka atubu, lakini tunaweza kumpenda, kumwombea na kumngoja huku mikono ya upendo ikiwa wazi. Baba yake mwana mpotevu hakusafiri kwenda nchi ya mbali kumpa mtoto wake mkopo wenye masharti nafuu, lakini pia alipomwona mtoto wake akirudi nyumbani kwa aibu hakumpa kisogo. Alimkimbilia akamkumbatia. Yusufu hakujitambulisha kwa ndugu zake walipomtembelea Misri mara ya kwanza, lakini walipoonyesha toba yao baadaye, aliwapokea kwa machozi.
Upande Wa Pili Wa Shilingi
Vipi kama wewe ndiye unayehusika kupokea hiyo adhabu ya kanisa? Ndugu anakujia kwamba umemkosea. Ufanyeje? Unatakiwa ujinyenyekeze, usikilize kwa makini na ufikiri anachosema. Ukifikiri hoja yake ni halali, tubu na uombe msamaha. Ukifikiri siyo, zungumza naye taratibu na ushughulike kutafuta maelewano na mapatano. Pengine utafaulu.
Kama atarudi na mmoja au wawili wengine, na waungane na huyo mlalamikaji baada ya kusikiliza upande wako, unatakiwa ufikiri kwa makini sana kile wanachokwambia, ukiri kwamba umekosea na uombe msamaha.
Kama unaamini kwamba wote watatu wamekosea na wapeleke jambo hilo mbele ya kanisa zima, unatakiwa ukubali kukutana na yeyote katika uongozi anayetaka mkutane. Eleza kwa makini upande wako, na kama kanisa zima litasimama na ndugu aliyekosewa, unatakiwa utambue kwamba una makosa, ukiri na kuomba msamaha.
Adhabu Ya Kanisa Kwa Kinyume
Adhabu ya kikanisa ni aina ya adhabu ya Mungu kwa kuwa inafanyika kwa agizo Lake. Ni njia nyingine anayotumia kutuhamasisha tuwe watakatifu, na ni njia anayotumia kulitunza kanisa Lake katika hali ya usafi.
Katika makanisa yaliyojaa Wakristo wa bandia, mambo ni tofauti kabisa. Mimi namjua mchungaji mmoja mcha Mungu aliyekataa kushirikiana kuimba na mtu aliyekuwa mshirika wake na ambaye alikuwa katika ndoa isiyo halali. Huyo mtu alitoka katika familia maarufu ya ‘vigogo’ hapo kanisani, na waliposikia hicho alichofanya mchungaji wao, walifanya mpango wa kumwondoa. Walisema kwamba alikuwa amezidi sana kuhukumu watu na alikuwa hawezi kuchukuliana na watu, na washirika wengi wakawaunga mkono. Mwishowe walifaulu kumwondoa. Hiyo ni adhabu ya kanisa kwa kinyume, na ni njia nyingine ambayo Mungu analitunza kanisa Lake kwa usafi!
Tunapaswa kufikiri juu ya yote matatu – kumpenda Mungu kwetu, matumaini ya thawabu na hofu kwamba tutaadhibiwa – kuwa ni ishara nyingine ya neema ya Mungu kwetu. Kila moja ni zawadi ambayo hakulazimika kutoa, lakini ameitoa, kwa neema Yake. Yeye apokee utukufu wote kwa utakatifu wetu!

0 comments:

Post a Comment